Monday, December 26, 2011

KUZUNGUMZA KWA UFASAHA

Maneno ya heshima, yaliyotamkwa kwa ufasaha huamsha hisia na kufanikisha tafakari. Ili kufanikisha mazungumzo; mazungumzo ya siku kwa siku, mzungumzaji anapaswa kupanga mawazo yake kabla ya kuanza kuzungumza.
Mbali na hilo; yafuatayo ni muhimu kuzingatiwa:

1) Kujipanga.
Ni vyema kupanga mawazo au hoja kabla ya kuanza kuzungumza. Mzungumzaji anapaswa kuweka mawazo ya msingi mwanzoni; na yawe katika mtiririko. Hii hufanikisha ufahamu kwa upande wa pili.

2) Kukaa kimya.
Kama mzungumzaji anahisi atakayosema yatamkwaza mtu; kama mzungumzaji anayo hasira ni bora akae kimya. Maneno ni kama mawe, pindi yanaporushwa hayazuiliki. Mzungumzaji asitishe anayokusudia kusema mpaka hali itakaporuhusu.

3) Kuwa muungwana.
Mtu (mzungumzaji) anapaswa kujenga tabia ya kutoa hoja kwa lugha ya upole. Kuonyesha uungwana na heshima dhidi ya upande wa pili; hufanikisha mazungumzo kwa urahisi pia, kuleta muafaka.

4) Kuepuka maneno "haijatokea" na " ni kawaida".
Kauli nyingi zinazoundwa na maneno hayo huwa hazina ukweli; pia ni vigumu kuzithibitisha. Maneno hayo hujenga jazba na hutatiza mawasiliano. Mfano, "ni kawaida yako kunihadaa", "haijatokea ukakubali mawazo yangu", n.k

5) Kusifia.
Ingawaje mzungumzaji anaweza kukinzana na hoja; lakini si 100%. Mzungimzaji anapaswa kutambua umuhimu wa mada; na ambao unafanya upande wa pili kutetea. Kisha mzungumzaji aanze kwa kuunga mkono au kusifia; na baadaye kutoa hoja zake za kukinzana.

Kwa mfano, "ni kweli kabisa! Lugha na historia ni vielelezo kwa taifa lolote lile, lakini vitu hivyo havichangii kukuza uchumi wa taifa. Kwani hata siasa, amani n.k havitegemei lugha au historia bali uchumi wa nchi husika".

6) Kukubali udhaifu.
Mzungumzaji asiongee kwa kujiamini hata akasahau madhaifu yake au alipokosea. Kuongea kwa kupitiliza hufanya upande wa pili kuhisi unashambuliwa; hivyo unaweza kupata jazba na hatimaye kuanzisha vurugu.

Mawasiliano bora yanapaswa kuleta au kukuza maelewano; wakati mwingine upande mmoja unaweza kutoridhika kutokana na kukubali haraka. Hali hiyo inaweza kuondolewa kwa:

1) Kutokimbilia kusema "Ndio"
Watu hukubali ilimradi yaishe. Kama mtu anahisi anao wasiwasi anapaswa kusema " nipe muda kidogo ili nifikiri juu ya hilo". Hivyo kupata muda wa kutafakari na kutoa jibu sahihi.

2) Kueleza hali halisi.
Kama mtu hana ujasiri wa kukataa; anapaswa kuleza hali aliyonayo, au changamoto zinazomkabili. Hii husaidia kupunguza upinzani pindi atakaposema "Hapana".

3) Kutoa mapendekezo.
Kama mtu yupo katika wakati mgumu; au akatae au akubali ombi la kushiriki jambo fulani, anapaswa kutoa mbadala au majina ya watu wanaoweza kufanya shughuli husika kwa ufasaha.

4) Kutolumbana.
Kama moyo na nafsi vinamwambia mtu asema "Hapana", basi asianzishe malumbano ikiwa kutotoa kwa kina sababu za kukataa; hususani kama alikwisha kueleza hali aliyonayo.

Kama upande wa pili unasisitiza au kuendekeza malumbano; mzungumzaji atumie busara. Mfano anaweza kusema "Tafadhali, nawasihi msinihinikize ili nilumbane, malumbano hubomoa misingi. Jibu langu ni HAPANA"

Monday, December 19, 2011

KUSIKILIZA KWA MAKINI

Kufanikiwa au kutofanikiwa kunafanikishwa na ubora wa mawasiliano. Mawasiliano bora humwezesha mtu kueleweka na kukubalika. Mawasiliano ni muhimu kwa mahusiano baina ya; mtu na nafsi, mtu na mtu, mtu na familia, mtu na marafiki n.k

Maneno tunayozungumza na kusikia hupelekea; faraja au huzuni, usalama au hatari, kukubalika au kukalika n.k. Mbali na maneno, ujumbe wa ishara (kama vile kutazama, tabasamu, kuchezeha kichwa, matumizi ya mikono n.k) unamadhara makubwa sana au sawa na maneno/sauti.

KUSIKILIZA KWA UFASAHA.

Jambo moja na la muhimu katika mawasiliano ya sauti ni KUSILIZA. Binadamu amepewa mdomo mmoja na masikio mawili ili.......... Umakini katika kusikiliza hukuza na kuboresha mawasiliano, humsisimua mzungumzaji na kumhamasisha msikilizaji.

Kufanikisha usikivu fasaha; yafuatayo ni muhimu:
1) Kufahamu lugha ya ishara.
Kuwa makini na matumizi ya viungo vya mwili vya mzungumzaji; kama vile mikono, miguu, kichwa, tabasamu n.k. Lugha ya ishara hutumiwa na mzungumzaji kuboresha ujumbe anaotoa na hivyo kuboresha mawasiliano.

2) Kuondoa vikwazo.
Ili kusikiliza kwa ufasaha, mtu ajitahidi kadiri ya nguvu zake zote kuondoa mawazo na changamoto zinazomsonga. Vikwazo vinaweza kuwa kelele, mtazamo hasi juu ya ujumbe n.k. Kuondoa vikwazo kunawezeshwa na kuelekeza mawazo pia kujenga taswira juu ya kinachozungumzwa.

3) Kuomba ufafanuzi.
Kama mtu hajaelewa ipasavyo; kama anao wasiwasi au kama hajaelewa baadhi ya maneno n.k; anapswa kuomba ufafanuzi. Komba ufafanizi kuwe kwa lugha ya upole na unyenyekevu, lugha ya ukali kama vile "kwani hauna sauti? "unaniongelea kama mgonjwa?", "mimi sikusikii" n.k huondoa hari ya mzungumzaji; na hivyo kusitisha mazungumzo.

4) Kuthibitisha ulichosikia.
Mawasiliano yoyote hutegemea mwitikio. Ili kuhakikisha kuna uelewano hususani mambo ya msingi; inampasa msikilizaji kuthibitisha alichosikia na kuelewa, anapaswa kutoa mrejesho kwa mzungumzaji.
Mrejesho unaweza kuwa ni ufupisho wa ujumbe au ufafanuzi kwa kadiri ya alivyoelewa. Mfano, Mzungumzaji: nitafute kesho saa moja.
Msikilizaji: nikutafute kesho saa moja ya asubuhi?

5) Kutambua hisia za mzungumzaji.
Hisia au hali aliyonayo mzungumzaji husaidia kujua aina ya ujumbe anaoutoa. Mtu anapaswa kujua sababu za mzungumzaji kuongea kwa lugha ya ukali, lugha ya upole, kuangalia chini au pembeni, kuongea mfululizo n.k. Kujua hisia husaidia kuchukua hatua sahihi ili kuelewa ujumbe.
BINADAMU AMEPEWA MDOMO MMOJA NA MASKIO MAWILI ILI, ASIKILIZE ZAIDI YA KUZUNGUMZA.

Monday, December 12, 2011

UBUNIFU.....unaendelea.

Hatua Tatu za Kuongeza Ubunifu.
1) Kuamini inawezekana.
Kuamini jambo unaloona ni gumu; ya kwamba linawezekana huweka akili katika mwendo (njia) kuelekea kwenye suluhu. Kuamini huimarisha misingi na mazingira kuelekea "kusadikika".

Mtu anapaswa kuamini katika vitu vinavyoonekana ni vidogo na havina msaada kwa kuwa, siri za mafanikio hazitegemei mambo makubwa na maajabu ili kufanikiwa.

2) Kuondoa neno "HAIWEZEKANI" katika matamshi.
Mtu anaposema sentensi fulani juu ya jambo fulani mara kwa mara, uhalisia wa anayosema hujitokeza katika matendo.
Pale mtu anapotamka jambo fulani haliwezekani kabisa au zaidi ya ubora fulani, huifanya akili kutochukua hatua zozote au za ziada.
Wataalamu wa akili wanasema, analosema mtu ni matokeo ya mawazo yake, na kwa kiasi kikubwa humtokea. Waswahili wanasema, mdomo huumba.

3) Kukubali kupokea mawzo mapya.
Kufungua akili na kukubali kupokea mawazo mapya ni kama kuongeza mbolea na maji kwenye mimea.
Mtu anapaswa kuchambua mawazo mapya kwa kina, na kwa kadiri ya mahitaji, kudadisi ni kwa nini na kwa vipi mawazo husika hufanya kazi.

Jinsi Gani ya Kuishi mbinu za Ubunifu?
1) Kutenga muda na eneo tulivu kwa ajili ya tathmini ya kila siku, kabla na baada ya kulala.
2) Kujenga mazoea ya kutumia akili kuliko nguvu katika kukabili changamoto.
3) Kujenga mazoea ya kuishi kwa kufuata mawazo mapya na si kuishi kwa mazoea.
4) Kufanya kazi na mazoezi ambayo huimarisha na kukuza seli za akili. Mfano, michezo ya kompyuta.
5) Kukuza vionjo na silika; kuacha kushangaa bali kufanya jitihada ili kinachoonekana au kuwazwa kitimie.

Pia mtu anapaswa kufahamu ya kwamba:
¤ Kipawa asilia hakiletwi na milango mitano ya fahamu tu, bali akili fichika (subconsious mind).
¤ Akili fichika inafanikisha ujenzi wa taswira ambayo hupokewa na milango ya fahamu ili kufanikisha ukweli.
¤ Ubunifu wote huletwa na akili fichika.
¤ Ubunifu huonekana baada ya kuweka misingi na kuwaza chanya juu ya maisha.

Monday, December 5, 2011

UBUNIFU

Ubunifu ni nguvu mtu anayoibua kutoka katika taswira, taswira ya kitu kinachoonekana. Ubunifu ni bora kuliko kuwa na maarifa kwani, maarifa yana kikomo ili hali ubunifu hutapakaa ulimwenguni kote, huchochea mabadiliko yanayozaa maendeleo.

Ubunifu ni kiunganishi kati ya kipawa alichonacho mtu na mchango ulimwengu unaotoa kwa mtu husika. Kila kinachoonekana na taswira yake huwekwa katika akili, baada ya muda hutekelezeka kupitia ubunifu.

Kuna aina kuu mbili za ubunifu, nazo ni;
1) Ubunifu sanisi.
Katika aina hii ya ubunifu; mawazo, fikra na mipango aliyonayo mtu hupangwa katika mfumo mpya na tofauti. Aina hii hutegemea elimu na uzoefu alionao mtuu juu ya fani fulani.

2) Ubunifu kipaji.
Aina hii huvuta hisia na maono pamoja, hujengwa na jinsi mtu anavyopokea na kujibu yale anayoambiwa na mazingira. Ubunifu huu hautegemei uzoefu alionao mtu, bali elimu kidogo juu ya nyanja fulani. Ubunifu huu ndio chanzo cha ugunduzi.

Jinsi ya Kijenga Ubunifu.

1) Kuchangamsha akili kwa kusoma.
Kusoma ndio njia ya kuaminika yenye kukuza vipawa na siri zilizofichika katika katika dunia.
Mtu anapaswa kusoma yale yanayonfanya afikiri kwa kina, yanayotoa changamoto juu ya imani ya mtu na kuonyesha njia fasaha ya kufuata. Kumbuka siri za dunia zimefichwa kwenye maandishi.

2) Kuendeleza maboresho.
Kila umbo la kitu kinachoonekana ni maboresho yatokanayo na taswira, taswira aliyokuwa nayo mtu kichwani juu ya umbo hilo.

Uendelezwaji wa maboresho unawezeshwa na mbinu sahihi za kupumzisha akili na mwili. Kila siku mtu ahakikishe anapata mahali kwa ajili ya kupumzika; mahali ambapo atakaa kimya; kufunga macho na kupumua huku akifikiri juu ya mwenendo wa siku inayoisha, inayofuata na maisha kwa ujumla.

3) Kuwa na lengo.
Mtu anapaswa kuwa na lengo pamoja na azma juu ya maisha yake; juu ya maisha ayatakayo.
Ili kufanya hivyo, mtu anapaswa kuvunja vunja na kuunga upya vipande vianavyojenga lengo na azma husika. Kufanya huvyo husaidia kuona mapungufu na jinsi ya kuyakabili kabla au wakati wa utekelezaji wa lengo husika.

4) Kuwa na nguvu za umakini.
Nguvu za umakini huletwa na ridhaa na nidhamu ya mtu, ridhaa na nidhamu ya kutaka kutekeleza kile anachoamini ni sahihi kwa manufaa yake na ya jamii nzima. Nguvu za umakini huwezeshwa kwa utizamaji wa kina juu ya lengo, matendo, mienendo na hisia kuelekea ufanikishwaji wa azma husika.

5) Kumiliki vionjo.
Tamaa na jazba ni visafiria vianyotumiwa na wahujumu ili kuleta vikwazo; kukatisha tamaa; kuondoa imani; kujenga hofu na hatimaye kutochukua hatua sahihi. Hujuma hushambulia nafsi zaidi, hujuma zinaweza kupunguzwa na kuondoshwa kwa jitihada za mtu kumiliki mawazo yake, mienendo na mitizamo kwa hali ya juu.

Ubunifu uhamasishwa na tabia ya mtu ya kufikiri na kudadisi juu ya njia mbadala na sahihi ili kupata suluhu rahisi katika kutatua changamoto inayomkabili mtu binafsi na jamii kwa ujumla

Monday, November 28, 2011

AZMA KATIKA MAISHA

Azma ni jumla ya mambo yote ambayo mtu anataka maisha yake yawakilishe. Azma ya mtu huendana sambamba na fani (kazi) ya mtu husika.
Ikumbukwe ya kwamba kinachoangaliwa na jamii (watu wengi) si wingi wa miaka aliyinayo mtu au uzoefu bali, ni mchango wake katika maisha ya jamii husika.

Maswali ya msaada (mwongozo) anayopaswa mtu kujiuliza wakati anapoamua azma ya maisha yake katika jamii yoyote ile.
1) Je nataka maisha yangu yaweje?
2) Je naishi maisha sahihi?
3) Je nafanya nini ili kufanikisha maisha sahihi?
4) Je nafanya nini kila siku ili ndoto zangu zitimie?
5) Je nimetoa mchango gani kwa jamii?
6) Je mchango niliotoa kwa jamii ni sawa na jamii ilivyoniwezesha?
7) Je maisha yangu yatajizatiti kwa lipi?
8) N.k

Vigezo Saba Wakati wa Kujenga Azma.

1) Kamilifu.
Mtu anapaswa kutazama vitu kama vitakavyokuwa, na si kama vinavyoonekana.
Kutazama kwa mapana na marefu juu ya kila wazo au lengo alilonalo mtu. Mtu anapaswa kutazama huku akiangalia baadaye, je anachowaza kitafanikiwa?
"Daima tazama juu nawe utakuwa juu"

2) Kuwa na mwanga.
Azma ya mtu lazima itazame mbele, mbele ya ombwe na mbali na upeo wa macho. Mtu anapaswa kujifunza jinsi ya kuitikia, kukumbuka na kukubali "ndoto".
Mwanga huu ni mapokeo ya juu na ya ki-ujasiri. Mtu anayo mamlaka ya kutengeneza taswira kutoka kwenye mawazo aliyonayo kupitia mwanga huu.

3) Kudumu maishani.
Azma ni taswira ya mtu inayowakilisha majukumu ya mtu katika ngazi tofauti-tofauti alizonazo katika jamii. Majukumu aliyinayo mtu yanapaswa kudumu hata kama mwanzilishi hayupo duniani. Sifa hii imewafanya watu wengi wailioondoka duniani kukumbukwa mpaka kesho. Mfano; Martin Luther King Jr, Mwl J K Nyerere n.k

4) Kunufaisha kila mtu.
Azma inayolenga kumnufaisha mtendaji ni ishara ya wazi ya ubinafsi wa hali ya juu, ubinafsi unaotishia usalama na uhai wa jamii.
Azma inapaswa itazame watu wote katika jamii, inufaishe makundi yote ya wanajamii kuanzia; watoto, vijana, wazazi, wazee n.k.
Mfano, je biashara, taaluma n.k yangu ni kwa ajili ya nani?

5) Kushawishi.
Azma inapaswa wakati wote ishawishi imani na uwezo wa mtungaji. Inapaswa imshawishi mtu kufanya kila jitihada zilizo halali lili kutimiza azma husika.
Mfano, kama mtu anataka kuwa mfugaji wa kuku, azma ya kufuga kuku imshawishi atafute msaada kutoka kwa wafugaji, wataalamu wa mifugo n.k ili kufuga kuku kwa ufanisi na si kwa mazoea.

6) Kuchoma.
Azma ya mtu iwe kama moto, moto unaochochewa na imani ya kufanikiwa. Imani ya kufanikiwa huwa kama moto unaoamsha hisia na uwezo wa akili pamoja na misuli kana kwamba, mtu anakuwa na ujasiri na uthubutu juu ya vikwazo vyote vya kibinadamu.

7) Kuwa na manufaa.
Azma ya mtu inapswa kutimiza matakwa ya jamii na dunia kwa ujumla. Iwe na uwezo wa kukabili na ktoa suluhu dhidi ya changamoto zinazomkabili binadamu kwa wakati husika.
Azma inayolenga kuondoa adha kwa jamii hupata msaada kutoka sehemu mbalimbali duniani. Mfano, je azma yangu ya kufungua mradi wa kilimo itapunguza tatizo la ukosefu wa ajira katika jamii yangu?

Monday, November 21, 2011

MALENGO

Malengo ni kama mstari unaotoa mwelekeo (dira) wa mahali anapotaka kufika. Malengo humpa mtu sababu za kujiamini, hususani kama yakitimia.
Kujenga tabia ya kuweka lengo humfanya mtuasonge mbele kuelekea kokote atakako.

Aina Za Malengo.
1) Malengo ya muda mfupi.
Malengo haya ni ya karibu. Huwakilisha mahitaji yanayopaswa kutekelezwa ndani ya muda mfupi, bila hata kutumia nguvu na rasilimali nyingi.
Malengo huchukua kati ya siku moja hadi tisini ili kutimia.

2) Malengo ya kati.
Malengo haya hutegemea malengo ya muda mfupi ili yatimie. Hutegemea nguvu kiasi ili kutimiza malengo ya muda mfupi. Malengo haya huchukua kati ya siku tisini mpaka miaka miwili ili kutimia.

3) Malengo ya muda mrefu.
Malengo haya hutegemea/ huhitaji vitu vingi ikiwamo muda na rasilimali nyinginezo. Huendana na fani ya mtu. Malengo haya huhitaji mikakati na rasilimali nyingi, pia kukamilika kwa malengo ya muda mfupi na wa kati.
Malengo haya huanzia miaka miwili na kuendelea.

Malengo yanaweza kuwa edelevu au pinzani.
Malego endelevu ni yale ambayo hutekelezeka hatua kwa hatua, huanzia na hali aliyo nayo mtu, huchochewa na mafanikio ya kila hatua ya ya mafanikio.
Kwa upande mwingine malengo pinzani ni yale ambayo hutaka mafankip ya ghafla, hukinzana moja kwa moja na hali aliyo nayo mtu.
Kwa ujumla, malengo endelevu hutekelezeka kwa urahisi yakilinganishwa na malengo pinzani
Sifa Sita za Malengo Yanayotekelezeka.
1) Kuandikwa na kushirikisha.
Kila lengo linapaswa liandikwe katika sentensi mbili au tatu. Malengo yaandikwe kwa lugha fupi na fasaha ili mtu aweze kukumbuka mara kwa mara.

Mtu anapaswa kuwashirikisha watu/ mtu ambaye anaelewa na kuamini katika lengo fulani. Mfano mfanyabiashara, mwalimu, daktari n.k. Ushirikishaji hulazimisha uwajibikaji, huleta ushirikiano, pia humsaidia mtu kupata msaada na faragha wakati wa kipindi kigumu.

2) Halisia na kufikika.
Malengo yanapaswa kuwa halisia na yenye kufikika. Ili lengo liwe halisia na lenye kufikika linapswa kuwekwa kwa kuangalia maendeleo aliyofikia mtu na rasilimali (viwezeshaji) alizo nazo mtu kwa wakati anapopanga. Watu wengi kuweka malengo bila kuangalia viwezeshaji kama ushauri, fedha n.k, hali hupelekea utekelezwaji duni wa malengo.

3) Kukubali mabadiliko.
Mtu anapoanza kutekeleza lengo husika, vikwazo na vizuizi huibuka kutoka pasipotegemewa. Lengo linapaswa kukubali mabadiliko pindi hali inapobidi.
Kwa mfano mtu anaweza kubadilisha aina ya biashara ndani ya muda husika kwa sababu kukosa fedha, kupatwa na ugonjwa n.k.

4) Kupimika.
Malengo ni matunda mtu anayoyarajia kupata kutokana na juhudi zake katika uwekezaji. Malengo yanapaswa yawekwe sambamba na vipimo ili kuweza kufuatilia utekelezaji. Vipimo vinapswa kuwa hatua kwa hatua, hii itasaidia kugundua wapi na vipi maboresho yafanwe kuligana na hali husika.

Watu huweka malengo bila vipimo hatimaye madhaifu mazito na yasiyorekebishika huonekena baada ya muda na rasilimali nyingiezo kutumika. Hali hii ianapelaea hasara isiyozuilika.
Kuwa na lengo bila kipimo ni sawa na kutembea njia ndefu inayoelekea mji fulani pasipo kujua ina uerfu gani.

5) kufuatata muda.
Kunapaswa kuwepo muda maalumu katika utekelezwaji wa kila kipengele. Muda hutumika kupima ufanisi. Muda unaopangwa unapaswa uende sambamba na ujuzi, rekodi ya mafanikio ya mpangaji au ya watu anaojifunza kutoka kwao, viwezeshaji n.k

6) Kuwa na lengo mbadala.
Lengo la mtu ni hali anayoitaka mtu baada ya wakati fuani. Kuweka malengo ya ziada (mbadala) hutoa njia mbadala ikiwa hali itakuwa ngumu kiasi kwamba inazuia utekelezwaji ya lengo kuu.

Mfano mtu anapanga kuuza nguo, kama nguo zikidorora afanye biashara ya nafaka. Lengo mbadala linapswa litumie mtaji, maarifa au rasilimali nyinginezo zinazoendana na lengo kuu ili kupunguza gharama na usumbufu wakati wa kubadili.

WATU WENGI HUPANGA KUSHINDWA, NA SI KUSHINDWA KUPANGA.

Monday, November 14, 2011

KUWA NA FURAHA LEO UFAIDIKE LEO!

Leo ni siku ya siku ya kuacha kuishi kwa kutegemea kesho. Kwani leo ni siku ambayo hautaishuhudia tena katika maisha yako, hivyo unapaswa kuifurahia hata kama ni chungu kama shubiri au mwarobaini.

Watu wengi huairisha furaha zao wakisubiri malengo yao yatimie ndipo wafurahie. Baadhi ya watu husema watakuwa na furaha ikiwa tu:
¤ watapata kazi nzuri,
¤ watakapopata wapenzi wa maisha,
¤ watoto wao watakapokuwa wakubwa,
¤ watakapohitimu masomo,
¤ watakapostaafu kazi za ofisini,
¤ n.k.
Watu hutoa sababu nyingi kama hizo zinazowapelekea kuishi kwa huzuni, huzuni wasiyostahili.

Kwa kawaida lengo moja linapofanikiwa ghafla malengo mengine huibuka hivyo, kumfanya mtu kuishi akisubiri furaha maisha yake yote. Inafaa kupambana ili kuwa na maisha mazuri huku akifurahia kila hatua ya mafanikio anayopiga kuelekea hayo "maisha bora"

Mtu anapaswa kujua ya kwamba wakati alionao (siku, saa na dakika) hataushuhudia tena katika maisha yake, ikipita imepita.
Yaliyotokea kabla ya leo na yatakayotokea kesho ni vitu vilivyo nje ya akili ya mtu. Hali halisi ni ile mtu anayoishuhudia wakati husika, wakati ambao anawezakfanya jitihada ili kuleta mabadiliko katika maisha.
Jiulize kama usipokuwa na furaha leo je utakuwa nayo lini?

Kuna njia rahisi ya kumfanya mtu afurahie (siyo aridhike) na hali aliyonayo mayo ni KUJITAMBUA.
Mtu anapaswa kutambua hali ya uchumi yake, jamii yake na yale yote anayoshuhudia ikiwamo changamoto. Kuangalia mazingira yanayomzunguka, kusikiliza kwa makini sauti ya moyo wake na kila kinachoingia akilini mwake.

Kutambua pale mtu alipo hufungua akili na furaha huchukua nafasi ya huzuni. Huzuni inayoletwa na mtizamo hasi kuhusu jana na kesho. Kujitambua huleta hisia chanya na kuonyeha viwezeshaji, viwezeshaji ambavyo husaidia kufanikisha malengo kwa haraka.

Ingawaje mtu hana uwezo wa kuzuia ukweli wa yale anayoshuhudia lakini, anao uwezo wa kumiliki anachoshuhudia ili kimsaidie. Mtu anapaswa kuita furaha na ikaja haraka hata asivyotarajia.

Kwa mfano, kama ntu anajikuta anawaza juu ya upungufu wa kiungo/viungo katika mwili wake, asitishe mawazo hayo na aanze kuamini mambo yatakuwa sawa ikiwa tu atapenda kwani, yeye si wa kwanza na wala hatakuwa wa mwisho. Wapo wengi, watu wengi wenye mapungufu makubwa lakini wamefanikiwa na kuwa watu muhimu katika jamii zao.

Kuna uhusiano mkubwa sana kati ya uwazaji wa mtu na homa. Mwili huathiriwa hasi na mfadhaiko wa akili. Maumivu yoyote ya nwili ni taarifa ya kwamba kuna kasoro na inahitaji suluhu.

Homa huibuka kwa sababu ya kupuuzia taarifa za mara kwa mara zinazotolewa na akili kuptia mwili. Hali inapokuwa mbaya ndipo mtu huchukua hatua za kubadili anavyowaza na kuanza kutibu maumivu.

Mtu anapaswa kuwa makini sana kwa kile mwili unachomwambia, pia kufahamu ya kuwa mwili na akili hufanya kazi pamoja. Akili ndio inayochukua hatamu za kuongoza mwili, ndiyo maana mtu akiwaza visivyo hupata homa ghafla.

Kama mtu atakuwa na mawazo chanya, anayotiba ya uhakika dhidi ya huzuni na homa. Tiba zote hutegemea hisia na mtazamo wa mtu (furaha) ndipo zitoe matokea ya haraka. Mtu anavyohisi juu ya jambo fulani, mfumo wa neva hutoa ishara zinazoathiri mfumo wa kinga ya mwili.
Kumbuka njia (kinga) bora katika kuzuia homa au kupunguza makali ya homa hata kama mtu anatumia dawa ni kuiamuru akili iite furaha.

Monday, November 7, 2011

UPWEKE

Mtu mwenye upweke hukumbwa na hisia za woga, woga ambao unazorotesha hali ya afya. Mara zote woga hujikita kwenye mahusiano ya mtu binafsi, mahusiano ya mtu na mtu/jamii, kazi, uchumi, afya na mustakabali kwa ujumla.

katika hatua za awali upweke unaweza ukamkumba mtu bila ya watu wengine kufahamu. Upweke na msongo wa mawazo ndio vikwazo vikuu kwa afya ya akili.
Kwa bahati mbaya hali ya maisha ya nyakati hizi huchangia kwa kiasi kikubwa tatizo la upweke pia hukuza ukubwa wa tatizo.

Jinsi ya Kuzuia Upweke.

Dalili za upweke hazionekani kirahisi, huonekana wakati tatizo limekua kubwa. Njia zifuatazo zinafaa ili kuepusha hali ya upweke.

1) Kuzungumza juu ya changamoto.
Kuzungumza na mtu sahihi ni hatua muhimu sana katika kutatua changamoto. Inafaa kumtafuta mtu wa karibu na ambaye anao uzoefu juu ya changamoto husika.

Watu wanaoishi peke yao (wenye kujitenga na marafiki, jamaa n.k) wapo katika hali mbaya zaidi, inafaa mtu kuwa na mahusiano mazuri na wale wanaomzunguka. Mawasiliano mazuri hufanikisha mazungumzo juu ya changamoto na huakikisha suluhu sahhihi inapatikana.

2) Mapumziko.
Kukosa au kuwa na mapumziko hafifu hukaribisha upweke, hivyo mtu anapaswa kupanga na kutumia muda hata kama ni kidogo kupumzisha mwili na akili.

Kuna njia nyingi za kufanya mapumziko kama; kutembelea wagonjwa, kwenda maeneo ya mbali, kufanya kazi za bustani, kuogelea n.k. Inategemea na muda mtu alionao, gharama, mapendekezo yake n.k

3) Kupumua.
Zoezi la kupumua ni rahisi na lenye mafanikio ndani ya muda mfupi. Kupumua hutumika kuondoa chembe za uchovu na upweke katika mazingira yoyote yale.

Zoezi lenyewe ni, kuvuta pumzi ndani taratibu huku tumbo (na si kifua) limetanuliwa, kisha kutoa hewa taratibu, zoezi lirudiwe mara tatu au nne mfululizo na mara mbili au tatu kwa siku, kadiri ya mapenzi ya mtu.

4) Kula sahihi.
Tafiti zimeonyesha ya kwamba kufungua kinywa kwa protini huondoa mawazo yanayofanana na upweke. Kufungua kinywa kwa protini kukifuatiwa na wanga, matunda n.k. Pia maji ya wastani wa glasi nane (inategemea na mazingira na aina ya vyakula) kwa siku.

5) Kujjihusisha na kikundi.
Inapaswa mtu kuwa katika aina yoyote ya kikundi, hususani kikundi kinachotoa mwamko, kikundi cha wakulima, wakina mama wajasiriamali,
n.k.
Katika kundi mtu anapata uzoufu kutoka kwa watu mbalimbali jinsi ya kupambana na changamoto za kimaisha. Hii inajenga ujasiri dhidi woga wowote ule.

6) Kutafuta habari kuhusu changamoto.
Mtu anapaswa kutafuta habari kutoka vyazo tofauti pindi anapohisi mambo hayaendi sawa. Kuna ushauri mwingi na wenye kufaa kwenye vitabu, majarida, CD/DVD n.k.

Habari sahihi huondoa wasiwasi kuhusu changamoto za kiafya, kikazi n.k. Kwa mfano mtu anaweza kupata ukweli juu ya vidonda vya tumbo, shinikizo la damu, kisukari n.k kwenye mtandao wa intaneti.

7) Kujiamuru.
Kujisemea maneno ya kutia moyo kama "hakuna kitakachotokea", naelekea kushinda", "Mungu wangu nipe amani, "Mungu uniodolee woga n.k kwa sauti na mahali tulivu.

8) Kuzuia mawazo.
Mtu anapaswa kuzuia mawazo yanayoleta woga au yanayoendana na woga. Mfano, mtu kuhisi anaugonjwa usio na tiba n.k. Mawazo kama hayo yanaonekana mapema, hivyo ni rahisi kuyazuia kwa kuyakataa.

9) Kuukabili woga.
Mtu anapaswa kumudu mbinu za kumpa ujasiri pale anapokumbana na hali tata na yenye kutisha. Hali aliyonayo mtu hutegemea jinsi anavyowaza hususani wakati wa changamoto, kukifuatiwa na uumbaji wa picha na baadaye upweke huota mizizi.

JIPIME
Jibu "N" kama jibu lako ni NDIO na "H" kama jibu lako ni HAPANA.
1) Je mapigo yako ya moyo yanaridhisha?
2) Je kama mtu akitaka kukukopa unashindwa kujibu "hapana"?
3) Je unapata jazba kwa mambo yasiyo na faida?
4) Je ni vigumu kusema "hapana" kwa muuzaji"
5) Je huwa unapata hofu bila sababu za msingi?
6) Je unaogopa sana na hali hiyo inakuuzunisha?
7) Je rafiki akikukosea unaweza kumwambia alivyofanya siyo sahihi?
8) Je unakataa au kuahirisha mikutano/mialiko?
9) Je mara zote unahisi kutoridhika?
10) Je unaweza kuhoji au kudai haki/stahili yako?
11) Je kama hujafikia muafaka na mpinzani wako unakaa kimya?
12) Je ni mzito kufanya maamuzi?
13) Je hutaki kupokea sifa?
14) Je mara nyingi unakuwa na hofu?
15) Je una uthubutu?
16) Je unaweza kuendelea na mazungungumzo na mtu baada ya kutofautiana?
17) Je unahisi kutoweza kutatua matatizo yako?
18) Je kama mtu akikupa upendeleo, unaweza kuukataa?
19) Je mara nyingi unafanya kazi kwa shinikizo?
20) Je kama hujaelewa kitu unaweza kuuliza hadharani?

UFAFANUZI WA MAJIBU.
¤ kama "N" ni kati ya 0 - 7, hauko kwenye hatari ya upweke.
¤ Kama "N" ni kati ya 8 - 12, upo kwenye hatari na unapswa kuchukua hatua (za hapo juu) ili kuweka mambo sawa.
¤ Kama "N" zaidi ya 12, ni mpweke, unapaswa kuchukua hatua na pia kumwona mwanasaikolojia kwa msaada zaidi.

Monday, October 31, 2011

NYAKATI KATIKA MAISHA

Mtu anapaswa kufahamu ya kwamba katika kukua kwake lazima apitie nyakati/ hatua tofauti. Ili kufahamu hilo mambo manne yanahitajika kueleweka kwa kina, mambo hayo ni yafuatayo.
Maisha ni bustani.
Maisha ni bustani ambayo ina maua mazuri (muelekeo chanya). Kama mtunza bustani (mtu husika) asipofanya jitihada kuondoa magugu (mawazo hasi) maguugu hayo huua maua.

2) Kila tendo lina matokeo.
Katika maisha kama mtu asipokuza kipawa alichopewa na Mungu vyema na kama mtu asipochukua hatua za makusudi kipawa chake kitatoweka.

Kwa kila analowaza na kutenda mtu lina madhara (ya kukuza au kudidimiza ) kipaji chake. Kama mtu akikaa kimya, ulimwengu humchagulia na daima humchaguila mabaya

3) Kila kitu kina wakati.
Maisha yana nyakati/ hatua, nyakati/ hatua ziko katika mtiririko. Nyakati zinadumu kwa kipindi cha miaka 20 -25. Kama mtu atashindwa kumudu changamoto za wakati haua fulani, mtu huyo atakuwa na kipindi mgumu sana mbeleni.

4) kuna kani mbili katika ulimwengu.
Takribani vitu vyote vinavyotokea katika maisha hutegemea nguvu za binadamu. Kila anchofanya binadamu huzaa wema au ubaya. Wema au ubaya ndio matokeo ya kazi za binadamu.

Hatua Anazopita Binadamu Katika Maisha

1)
Wakati wa elimu
Hii ni hatua ya kwanza, hatua hii huanza mwaka 0 mpaka 20 - 25. Katika hatua hii binadamu hujifunza misingi na kanuni muhimu za maisha. Mtu hujifunza kwa kusoma, kuandika, kuhesabu, kufikiri na kufanya maamuzi.

Mtu hujenga taswira binafsi, kujiamini, imani, woga, ujasirii n.k. Mtu hupata elimu/ ufahamu kutoka kwa wazazi/ walezi, waalimu, au mtu yeyote aliye karibu.
Kama hatua hii itajengwa kwenye misingi imara ya ukweli, uungwana, nidhamu, upendo, n.k hakuna kitakachomshinda mtu maishani.

2)
Hatua ya hisia na mihemko.
Hatua hii ya pili huanza miaka 20 - 25 mpaka miaka 40 - 50. Katika hatua hii mtu huanza kukumbana na changamoto za maisha, channgamoto za utu uzima kama mapenzi, vilevi, kazi n.k. Watu wengi huangusha/ kushindwa na hatua hii. Katika hatua hii tabia zinaweza kumjenga au kumbomoa mtu.

Wanaume huangushwa na hisia zinazoletwa na ulevi, mapenzi, kutaka kutawala n.k. Ili hali wanawake huangushwa na hisia zinazoletwa na kutaka kupata utulivu wa kimapenzi (kupendwa)

Ili kumudu hatua hii mtu anapaswa kujenga programu ya kipato, programu ambayo itamhakikishia mapato hayazidi matumizi. Mipango yote ya pesa ibajetiwe, kuwe na fungu la matumizi ya kawaida na la uzalishaji (uwekezaji au kukuza kipato). Mtu atumie fursa zinzotolewa na makampuni kama kununua hisa, biashara ya mtandao, kununua fedha za kigeni n.k ili kumhakikishia kipato siku za baadaye.

3)Hatua ya kuwa na nguvu.
Hatua hii ya tatu huanzia miaka 40 - 50 mpaka 60 - 65. Katika hatua hii mtu hufikia hatua ya hali ya juu ya mafanikio au kushindwa.
Mtu huonyesha kumudu au kutomudu mbinu za kufanikiwa.

Changamoto kubwa katika hatua hii ni kuchagua kuwa mwema au mbaya. Watu hulazimika kurudia masoma ambayo hawakuyamudu katika hatua za nyuma. Hupata changamoto ya kukabiliana na misukosuko ya kimaisha ambayo inahitaji nguvu nyingi na suluhu la haraka.

4)
Hatua mgando.
Hatua hii huanza mika 60 - 70 mpaka 100 na kuendelea. Mtu huchanganua alichofanya na kuvuna katika kuishi kwake, hutafuta mbinu za kufanya matunda ya kazi zake yadumu milele hata milele.

Mtu hutaka kuona kazi za mikono yake hazifi na ndoto zake zinadumu daima. Hali hiyo husisimua nguvu za nafsi, mwili na akili kwa kiwango cha juu. Mtu haogopi wala kutishwa na changamoto zinazomkabili na yuko tayari kufa akipigania anachotaka.

MIAKA ILIYOTUMIKA NI YA WASTANI KWA WATU WALIO WENGI, KWA BAADHI YA WATU BAADHI YA HATUA HUCHUKUA MIAKA MICHACHE SANA LAKINI WATU WOTE HUPITIA HATUA ZOTE.

Monday, October 24, 2011

NJIA 12 ZA KUKUZA TASWIRA BINAFSI

Ili kukuza na kuimarisha taswira binafsi, inampasa mtu kutumia njia zifuatazo wakati wote wa maisha yake hata kama atapata mafanikio mapema.

1) Kuwa mwaminifu.
Yapasa mtu kuwa mwaminifu, uaminifu unaoanzia moyoni. Yapasa kuweka nadhiri ya uaminifu kati ya nafsi ya mtu na yale ayatakayo (malengo).

Hii itamfanya mtu kuwa makini wakati wote anapohusiana na jamii inayomzunguka, vitendea kazi, na mazingira husika.
Ili kuona ukuu na umuhimu wa kutofanya makosa ya kizembe.

2) Kujenga taswira.
Taswira ni ramani au picha ya yale mtu ayatakayo, ni hatua ya kwanza katika uumbaji.
Taswira ya matarajio inaweza kujengwa kwa kusoma, kujihusisha na watu wanaoona vyema mbele na ambao wanaoweza kukuza ufahamu.

3) Kupumzika.
Kupumzika ndio moja ya njia sahihi ya kupunguza/ kuondoa msongo mawazo.
Mtu anaweza kupumzika kwa kwenda mazingira taofauti na yale aliyoyazoea, kuomgea na watoto wadogo n.k

Msongo mawazo hupunguza nishati na kinga ya mwili na kupelekea ugonjwa. Ugonjwa unashusha / unapunguza makadirio ya mafanikio.

4) Kuwa na imani ya ushindi.
Imani a ushindi ni hisia kali anayokuwa nayo mtu juu ya kukamilisha kitu fulani na kuona matunda yake.

Imani ya ushindi huonyeshwa na jinsi mtu anavyoongea, anavyotenda na anavyoishi.
Imani ya ushindi huvuta hisia za watu, watu huwa tayri kutoa msaada wa hali na mali ili kufanikisha malengo ya mtu husika.

5) Kujenga tabia njema.
Tabia na mienendo hukua na kuimarika baada ya muda mrefu, baada ya urudiaji wa mara kwa mara kwa mara.
Tabia jema ni zle zinazopelekea: afya njema, mapumziko sahihi, mlo kamili, mazoezi ya mwili na uwazaji sahihi.
Mtu hujenga tabia, tabia humjenga mtu.

6) Kuamua kuwa na furaha.
Kuwa na matarajio mazuri kila siku, kutarajia kila siku kuwa ya furaha huamuliwa pindi mtu anapoamka na kutaka kufanya kila kitu kwa amani.

Kudhamiria mema na mazuri wakati wote. Kama mtu atdhamiria kila siku kuwa njema, basi mtu huyo hujenga usumaku na mema aliyoyatarajia.

7) Kujivua gamba.
Gamba ni hali inayomjenga na kumlinda mtu dhidi ya watu wengine.
Lengo lake ni kuficha hali halisi ya mtu husika.
Ni kama uigizaji kana kwamba mtu anavaa husika usio wake. Mfano masikini kutumia pesa kidogo alizopata na watu matajiri na maarufu ili kuficha umasikini.

8) Kuwa na hisani.
Lazima kutambua hali halisi, matatizo na mahitaji ya wengine, na kuwa tayari kutoa msaada.
Mtu anapaswa kusaidia wenzake ambao hawajafanikiwa baada ya kupita hatua kulani ya mafanikio.
Kufanya hivyo humweka mtu karibu na Muumba na huinua utu wa mtoaji na mpokeaji.

9) Kuimarika kutokana na makosa.
Makosa ni masomo kimaisha kwa wenye busara.
Mtu anapaswa kujifunza kupitia makosa ya wengine (ili asianguke walikoanguka wanzake) na sio kufanikiwa kwao.

Pia kujifunza kupitia makosa aliyoyafanya mtu kwa uchambuzi wa kina ili kupata sababu za kukosa.
Kutumia makosa (yako na ya wengine) kama njia kuelekea mafanikio.

10) Kukubali udhaifu.
Kama mtu hatakubali udhaifu alionao kamwe hawezi kuushinda. Mtu asipokubali madhaifu yake hawezi kujua chanzo chake na hawezi kuchukua hatua za makusudi ili kuweka mambo sawa. Kutokubali kushindwa lili kujipanga zaidi hukuza ukubwa wa tatizo.

11) Kujikubali.
Kama mtu hatajikubali/ kuikubali hali yake au mtu atajifananisha na watu wengine, basi mtu huyo hutaka kujitenga na hali yake, nguvu zake na hisia zake.
Mtu ambaye hujikataa (hujisaliti) hawez kujua yeye ni nani na ana thamani gani.

12) Kuendelea kukua.
Maisha ni mchakato wa kupitia furaha, huzuni, magumu, changamoto n.k
Mtu anapaswa kukua kwa kpitia uelewa wa kina na uthubutu wa kufanya maamuzi, hasa maamuzi magumu (maamuzi yanayoamua mustakabali wenye heri) wakati wa changamoto.

Wednesday, October 19, 2011

TASWIRA BINAFSI

Taswira binafsi ni jinsi mtu anavyojifafanua mbele za watu. Ni picha ya mtu binafsi anayoionyesha mbele ya watu wengine. (mimi ni nani?).
Taswira binafsi inampa mtu uwezo wa ktoa, kupokea na kukabiliana na changamoto za kimaisha.

Taswira binafsi inayojengwa kwenye misingi ya woga, wasiwasi, kutokujiamini n.k huonyeshwa kwa hisia hasi.
Taswira binafsi iliyojengwa kwenye misingi ya upendo, heshima, imani, uelewa n.k huonyeshwa kwa hisia chanya.

Vitu Vinavyoathiri Taswira Binafsi

Kuna viti vitatu vikuu vianavyoathiri taswira binafsi ya mtu.
1) Mawazo na hisia wakati wa utoto.
Katika miaka saba ya kwanza, watoto hujenga mfumo wa kuthaminisha na ambao huongoza maisha yao yote.

Watoto hupenda na kutafuta mafundisho mazuri, mawazo mazuri, hisia nzuri na mienendo chanya.
Kwa bahati mbaya, hawana kinga dhidi ya mawazo mabaya, mafunzo mabaya na mienendo hasi.
Kwa kutokuwa na uwezo wa kuzia maovu, mawazo na matendo ovu huwatawala na kudumaza ukuaji wa taswira binafsi iliyo bora.

2) Mazingira
Mazingira yana mchango mkubwa sana, kwani ndio chanzo cha uthibitisho wa yote mtu aliyojifunza utotoni.
Mtu anapokuwa katika mazingira fulani kwa muda mrefu huchukua/ kufanana na tabia za mazingira husika.

Kamataswira ya mtu inakinzana na mazingira husika, kuna machaguo matatu:
¤ kubadilisha mazingira
¤ kubadilisha taswira binafsi
¤ kuondoka katika mazingira.

3) Makundi.
Makundi huleta ufanano. Makundi chanya husaidia kukuza taswira binafsi kwa; kuchambua mambo kwa kina, kukuza uelewa, maana n.k
Makundi hasi hudumaza taswira binafsi ya mtu kwa; kuzuia kutafuta habari, kuzuia kufikiri, kusistiza "haiwezekani" n.k.

Tabia Tano za Watu Wenye Taswira Binafsi Iliyo Duni.

Watu wenye ufinyu wa taswira binafsi ni wengi, kwa bahati mbaya zaidi wengi wao ni vijana.
Watu hawa wana/huonyesha sifa zifuatazo.

1) Kukwepa majukumu.
Watu hawa hukwepa kuchukua majukumu yao, hukwepa wajibu au matokeo ya yale waliyoyafanya.
Kwa mfano, mvulana anaposababisha ujauzito na kuamua kumsaliti msichana husika.

Kama mtu asipochukua majukumu yake, kamwe hawezi kubadili hali aliyonayo hata kama anaichukia sana. Mfano, mtu hawezi kupata mafanikio ikiwa ataacha kufanya kazi kwa bidii na kubaki kuilaumu serikali tu.

2) Kukimbia changamoto.
Mtu anapokumbana na changamoto, kuna machaguo matatu; kupambana, kusahau, na kukimbia.
Mtu mwenye ufinyu wa taswira huamua kukimbia changamoto husika. Mfano, kijana anapoamua kukimbia nyumbani baada ya kutofautiana na wazai/ walezi.

Mtu ataimarika kama tu! Atakabiliana na changamoto husika. Kukubali na kukabili changamoto huleta ujasiri na imani na kumwezesha mtu kukabliana na changamoto nyingi zaidi.
Je mtu atakimbia chanagamoto ngapi ili afanikiwe?

3) Kukosoa muada wote.
Watu wenye upumgufu wa taswira hutafuta mtu/watu wa kukosoa pindi makosa yanapotokea.
Watu hawa hukosoa kila kitu bila hata kuonyesha chembe ya kujenga, uungwana, heshima n.k.

Kukosoa kwa chuki hubomoa sio tu mkosolwe bali hata mkosoaji.
Kukosoa kunakojenga huambatana na upendo, heshima, utu n.k. Husaidia kujenga na kuimarisha watu wenye mapungufu. Huwafanya watu (mkosoaji na mkosolewaji) wakubalike katika jamii husika.

4) Husubiri watu watoe suluhu ya changamoto.
Watu wenye taswira binafsi duni hukaa na kusubiri rafiki, ndugu n.k watoe suluhu ya changamoto zinazowakabili. Kwa mfano, kijana anasubiri wazazi wamtafutie kazi.

Kama mtu atasubiri watu wampatie majibu ya changamoto zinazomkabili, mtu huyo kamwe hawezi kukua na kuimarika kwani kufanikiwa au kutaofanikiwa kunamuimarisha mtu.

5) Kupuuzia mambo.
Watu hawa huishi kana kwamba kila kitu ni sawa (OK!). Hujisahaulisha changamoto zinzowakabili. Huona hakuna haja ya kuwaza mbinu mbadala ili kuboresha hali husika. Huamini kila kitu ni sawa na inatosha, hakuna haja ya kuumiza kichwa zaidi.

Mfano, mtu anagundua amekosea moja ya hatua katika kufanya kitu fulani, kisha anajisemea haina tatizo, hata fulani alikoesea n.k. Hachukui hatua ili kurekebisha hatua husika hata kama anao uwezo wa kufanya hivyo.

Monday, October 10, 2011

SIRI RAHISI INAYOWASHINDA WENGI

Je, unayotabia ya kuandika malengo na kuyafanyia kazi? Kujiwekea malengo ndio mbinu kuu na sahihi ya kufikia mafanikio yoyote yale! Mbinu hii hutumika katika katika mipango yote, ya muda mfupi na muda mrefu. Kuandika matarajio ni kama kuchora ramani ya njia kuelekea kule mtu anakotaka kufika.

Kuandika malego kumewafanya watu wa kawaida kuwa watu mmarufu na muhimu katika jamii, vivyo hivyo kutoandika matarajio kumeshusha vipawa vya watu wenye uwezo.
Watu wengi wanajua ya kwamba kuandika malengo yao ni hatua muhimu kuelekea kwenye mafanikio yoyote yale lakini hawafanyi hivyo.

Kazi ngumu na yenye manufaa ni "kuamua". Inahitajika nguvu kidogo kufamya mambo makubwa lakini inahitajika nguvu kubwa kuamua mambo makubwa. Kufanya maamuzi ni kazi ngumu na inaathiri maisha ya watu wote. Kuwa mtu sahihi hutegemea maamuzi sahihi.

Mtu anahitaji zana sahihi ili kufikia malengo. Zana hizo ni KALAMU na KARATASI. Watu wako tayari kutembea umbali mrefu ili kukwepa kazi ya kuandika, wanaweza kuwaza, kuongea n.k lakini hawako tayari kuandika.

Hii ni kwa sababu kuandika kunahitaji kuwaza kwa kina. Kama huamini, jaribu kuanika chochote ndani ya sekunde kadhaa bila ya ya kufikiri.

Kuandika kuna nguvu mara kumi zaidi ya kuongea. Kuandika kunaanmsha seli za ubongo zilizolala na kumlazimisha mtu afikiri kwa kina na kwa ufasaha.

Kama mtu hajandika malengo yake, basi afahamu ya kwamba hayuko makini (serious). Kuwaza bila kuandika hufutika baada ya dakika chache lakini kuwaza na kundika hakufutiki kamwe!

Kitendo cha kuandika unayotaka ni kama kuwasha sakiti ya umeme kunavyopelekea taa kuwaka, mashine kufanya kazi n.k. Nusu ya tatizo litakuwa limepatiwa ufumbuzi kama mtu ataandika mbinu anazoamini ndio sahihi na jinsi ya kuzitekeleza.

Kuandika huleta nguvu ya ajabu inayoondoa woga, inayoleta matumaini na ujasiri. Kuandika malengo kunamfanya mtu kuchukua hatua ili kuyafikia, hubadilisha mtizamo na muonekano wa mtu husika.

Kuandika malengo kunagharimu dakika chache, huokoa zaidi ya miaka ishirini ya kuwa na matrajio (ndoto).
Kuona malengo yaliyoandikwa kwenye karatasi kunagonga kengele inayomtaka na kumlazimisha mtu kufanya jambo lolote ili kufikia lengo/malengo.

Mtu anatakiwa kujiwekea lengo/ malengo machache ili iwe rahisi kuyafanyia kazi mfano; "nataka kuwa mwandishi", "nataka kuwa mfanyabiashara" au "nataka kuwa mkulima" n.k.
Lengo /malengo hayo yaandikwe na kuwekwa sehemu tofauti-tofauti ambazo ni rahisi mtu husika kuona na kusoma mfano; kitandani, mezani, jikoni, mfukoni n.k.

Kisha lengo/malengo yasomwe kila siku asubuhi na jioni (kabla na baada ya kulala), huku mtu husika akiwaza kufanya jambo lolote siku inayofuata ili kufikia lengo.
Mtu anahitaji kukumbushwa zaidi kuliko kufunzwa.

Mbinu nyingine zinazohusiana na kuandika malengo ni:
-kujiambia kwa sauti katika maeneo tulivu "nitafanikiwa"
-kuangalia mafanikio ya watu waliokuwa na lengo/malengo sawa
-kusoma machapisho ya watu waliofanikiwa mara kwa mara
-kuongea na watu sahihi na wenye malengo sawa
-kusoma machapisho juu ya lengo lako
-kusikiliza mihadhara, radio, CD n.k
kujihusisha na watu wenye mafanikio.

Monday, October 3, 2011

HATUA SITA ZA KUWA JASIRI

Watu wengi wana uwezo wa kufanya mambo makubwa na yenye kuleta mafanikio, wanakosa mafanikio kwa kuwa hawana ujasiri wa kuwaza na kufanya maamuzi.
Njia zifuatazo zinasaidia kuimarisha uwazaji na kuwezesha kuchukua hatua zitakazowezesha kufikia malengo.

Hatua Ya 1: Chukua Hatamu Ya Maisha Yako
Kujali kile watu wanachosema juu yako ni kuwapa nafasi watu wayaongoze maisha yako badala yako.
Kujali watu wanachowaza ni utumwa unaowakabili watu wengi. Wengi tumelelewa (kwa nia njema) tukijali mawazo ya wengine zaidi, kitu kinachopelekea kuwa katika maisha, kazi n.k yasiyo na furaha wala mafankio.

kutaka kuwaridhisha wengine wakati wote ni tatizo linaloanza utotoni ili kukubalika. Hali hii huimarika ukubwani kiasi kwamba mtu anakosa kujiamini na kutanguliza mbele kile wanachowaza wenzake na si matakwa au mahitaj yake. Hali hii hupelekea umasikinii wa mawazo na hatimaye wa kipato.

Kabla ya kufanya chochote , jiulize, je unafanya kwa makusudio yako au ili kuaridhisha marafiki, ndugu n.k?
Kufuata mawazo ya wengine kunamfanya mtu kuwa; mtumwa, kunaua ubunifu na kumaliza nguvu za kutekeleza malengo binafsi, kunazuia mtu kwenda anapotaka, kufurahia anachotaka na hatimaye kukosa mafanikio anayotaka.

Hatua ya 2: Jitahidi Kuwa Tofauti
Karibu kila mtu anajitahidi kuwa sawa (sawa na marafiki, tabia, tamaduni n,.k) ili apate kukubalika katika jamii husika.
Inapasa mtu kuchambua mienendo yote kwa kina kujua kama "usawa" anaoutaka utaleta mafanikio au la!
Kama ni wa kufuata mkumbo, hatua za haraka zichukuliwe ili kuepusha utumwa au utekwaji nyara na mambo yatakayorudisha nyuma jitihada za kimaendeleo.

Hatua ya 3: Tazama Mbele
Ikiwa mtu atabaki kulaumu makosa aliyofanya awali, ajue anaua kujiamini na kushindwa kusonga mbele. Makosa ni mazuri (mtaji) kama yatachambuliwa ipasavyo (yakichambuliwa chanya au kama somo)

Kama mtu anataka kuwa jasiri, asichukue makosa kama makosa bali, kama masoma muhimu katika maisha. Hii itasaidia kujenga mustakabali wenye mafanikio.
Ili kufanikiwa haipaswi kukatishwa tamaa na idadi ya makosa. Kukosa ni muhimu ili kujua nini cha kufanya au kutofanya wakati fulani. kufanikiwa au kutofanikiwa ni suala la kimtazamo.

Hatua ya 4: Amini "Bado Sijachelewa"
Kuna watu wengi hawapendezwi na kazi wanazofanya kwa muda mrefu, lakini wanakosa ujasiri wa kuziacha kwa kuwa wanahisi wamechelewa kuanza au kujifunza fani/kazi nyingine.

Kama mtu analo lengo fulani, lakini anajikuta akijiambia "nimechelewa", njia pekee ya kuvua woga huo na kuvaa ujasiri ni kutouzingatia na kukabili kile anachokiogopa kwa nguvu zote.

Hatua ya 5: Kutojiwekea Ulinzi
Kuna wasomi wengi wamekosa mafanikio kwa kuwa kila wanachowaza kufanya wanawaza kwa tahadhari ya hali ya juu. Hali ambayo inawanyima uhuru.

Kuna watu wanaoweza kufanya biashara lakini hawana ujasiri wa kuthubutu, wanaogopa hasara kama kuwaka moto, kuibiwa n.k hivyo hutumia muda mwingi kufikiria juu ya kampuni za ulinzi, bima au tahadhari nyingine.

Ili kuepuka kujiwekea ulinzi uliopitiliza inapaswa kuthubutu. Kuthubutu yafutayo:
¤kuthubutu kuwa kuwa peke yako
¤kuthubutu kuwa na mtindo wako wa maisha na si kufuata mitindo ya kundi fulani bila sababu za msingi
¤kuthubutu kusoma na kufanya kazi kwa bidii ili kuimarisha fani husika
¤kuthubutu kuwa na mtazamo chanya na ujasiri wa kujaribu.

Hatua ya 6: Amini Utafanikiwa
Daima dumu! Kufanikiwa au kutafanikiwa kunategemea mtu anavyowaza na kuamini. Hivyo ili kuwa na ujasiri mtu anapaswa kuamini kwamba kuna kufanikiwa, huku akifanya mambo yanayopelekea mafanikio.

Ili kuvunja minyororo na utumwa wa mawazo "nitashindwa" yafaa:
¤kuchati chanya kimoyo-moyo
¤kujihusisha na watu wanaowaza kufankiwa au waliofanikiwa
¤kuwaza "nami" naelekea kufanikiwa
¤kuwaza "mimi" ni mshindi.

Mtu anapaswa kujishawishi yeye mwenyewe. Watu humshauri mtu juu ya kufanikiwa baada baada ya yeye binafsi kujishauri.

Monday, September 26, 2011

UWAZAJI CHANYA

Je umewahi kujiuliza, kwa nini kuna hisia tofauti- tofauti juu ya janga fulani? Kwa nini majanga kama kupoteza ndugu, mafuriko, n,k upokewa kwa hisia tofauti na wahanga?

Hii ni kwa sababu watu hupokea na kuchambua taarifa kwa namna tofauti, wengine chanya na wengine hasi.

Watu wanaochukua majanga kwa mtazamo chanya wanafaida zifuatazo:
-huimarisha mahusiano yao na jamii inayowazunguka
-huongeza ufanisi katika taaluma, kazi n.k
-huimarisha kinga ya mwili
-hupunguza maumivu ya ajali na majeraha mengineyo

Je Mtu Anawezaje Kuwaza Chanya?

Kukataa mawazo hasi ni hatua muhimu na ya awali kwa mtu yeyote anayetaka kuwa na furaha na ustawi maishani.
Uwaji chanya unafaa uwe wa kudumu, na si wakati wa matatizo au baada ya ushauri kutoka kwa wanasaikolojia na wataalamu wa akili.

Ili kuwaza chanya, yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa kipindi chote cha maisha ya binadamu.

1) Uwazaji chanya juu ya mtu binafsi.
Epuka kuishi kwa kujilinganisha na watu maarufu kwenye TV, jamii n.k.

Kipimo cha mafanikio kiwe ni malengo na si mafanikio ya wale uliozaliwa nao, uliosoma nao, uloanza nao kazi n.k.
Yakubali mapungufu yako, na dhamiria ili hayo mapungufu yasitokee tena maishani.

2) Kuwaza chanya juu ya yaliyopita.
Historia haibadilishwi, ikubali hata kama ina chembechembe nyingi za uchungu.
Kuilaumu historia kana kwamba ndiyo iliyopelekea hali ngumu uliyo nayo haisaidii chochote!!
Mfano, kama baba angenipeleka shule...., kama fulani asingenisaliti... n.k

Kumbuka yote mazuri yaliyotokea nyuma, yatakusaidia na kukupa ujasiri wa kufanya maamuzi.
Kwa mfano, wazazi wamenipa malezi bora, kusalitiwa kumeniimarisha n.k
Kumbuka mawazo, mitizamo na mawaidha ya wazazi, marafiki n.k ingawaje hawapo duniani.

3) Kuwaza chanya juu ya yajayo.
Kesho inatengenezwa na mitizamo yako ya leo. Ukiwaza kwa ujasiri na kijiamini kuhusu kesho kunaongeza uwezekano wa kufanikiwa.

Hata kama changamoto zitatokea utaweza kuzikabali, kuwa na mipango sahihi bila ya malalamiko na hasira.
Mfano, nimefeli mtihani! Akili imefunguka na ntasomea ufundi kisha kujiajiri binafsi.

4) Kuwaza chanya juu ya watu na mazingira.
Kumbuka hakuna kilichotimilifu, ila kuna mema na matamu katika kila mtu na mazingira.

Usijenge hasira juu ya watu na mazingira fulani, amini watu na mazingira huku ukifanya jtihada kukabiliana na changamoto.

Jitahidi kuelewa kwa undani watu na mazingira husika.
Jiulize je, ni watu wote walio katika mazingaira fulani (mfano mijini) wamefanikiwa?

Jenga imani na wote wanaokuzunguka (marafiki, ndugu, majirani n.k) na kuchukua mawazo na changamoto wanazotoa kama mtaji kwako. Na hatiamye.

5) Mshirikishe Mungu.
Jaza moyo wako mawazo ya kiimani kwa kumtanguliza Mungu, kwani dini (imani) zote zinajenga utulivu wa akili.
Amini ya kwamba kufanikiwa ni kwa ajili ya binadamu wote, watu wote ni sawa mbele ya Mungu. Mruhusu Mungu akupe silaha na nguvu za kupambana na hila zote kutoka kwa waovu.

Monday, September 19, 2011

Mawazo Yako Ndio Mtaji Wa Maisha Yako

Upo uhusiano mkubwa sana baina ya namna mtu anavyofikiri na jinsi anavyoishi. Kushindwa kwa mtu hakutegemei nguvu yoyote aliyonayo isipokuwa ufahamu wa mtu husika.
Kuanguka kwa mtu hakutegemei idadi ya maadui aliyonao, isipokuwa aina ya mtazamo aliyonao. Kurudi nyuma kwa mtu (kiuchumi, kijamii n.k) hakutegemei historia aliyowahi kuwa nayo mtu husika, isipokuwa uendekezaji wa mawazo ya kushindwa.

Binadamu huongozwa/hujengwa na mawazo, mawazo ambayo yanapatikana katika mazingira husika.
Kwa kawaida mtu anapoona, anaposikia au jambo linapomtokea yeye mwenyewe, akili yake humpa tafsiri tofauti-tofauti juu ya jambo husika. Fikira hizo zinampa mtazamo fulani (- au +) katika maisha yake.

Mawazo hayo, baada ya muda huwa yanajitokeza katika maneno yake na hata katika matendo yake. Hivyo mtu huzugumza kufanikiwa au kutofanikiwa na baadaye kukifuatiwa na matendo.

Ni sawa na kusema kufanikiwa au kutofanikiwa ni suala la kimtazamo kuliko kuwa nacho au kutokuwa nacho.
Mifano ya kufanikiwa ni kama kuwa na; marafiki, upendo maadili mema n.k. Kwa upande mwingine kutofanikiwa ni kama kuwa na; huzuni, umasikini, maadui, n,k. Mawazo ndiyo asili ya hali inayoonekana kwa nje.

Kuna mifano michache:
¤Mark (26) aliamini anaweza kufanya biashara lakini hajui pakuanzia. Siku moja alihudhuria semina yenye lengo la kujenga uwezo wa vijana juu ya ujasiriamali.
Mazingira ya ukumbi, ufasaha wa lugha kutoka kwa wahadhiri, mifano halisi kutoka kwa wajasiriamali wazoefu n.k viliamsha hari ya Mark juu ya kuanzisha biashara.
Kuanzia hapo, Mark akatafuta ushauri zaidi, akatembelea maduka ya jumla, akatafuta mtaji kutoka kwa marafiki zake kisha kuanzisha biashara ya kuuza viatu vya mtumba.
Biashara ambayo imebadilisha maisha yake na ya familia yake.

¤Halima (27) alitoka kwa chakula cha jioni na rafiki zake watatu aliosoma nao high school.
Walifurahia mazungumzo, mazungumzo yaliyohusu mambo na matukio muhimu katika maisha ya sekondari, chuo na hata kazini.
Katika maongezi na michapo na michapo, Halima akaoanisha maisha yake na yale ya rafiki zake ndani ya miaka nane. Hatimaye akaona ya kwamba rafiki zake wanabahati zaidi yake. Ghafla akakumbwa na huzuni ukifuatiwa na msongo wa mawazo na kukosa usingizi kwa siku kadhaa.

Mtu akitaka kubadili hali yake (ya uchumi, mahusiano, kazi n.k) anapaswa kudhibiti yote anayoyaona au kusikia juu ya hali yake ya sasa, pamoja na hayo anahohubiriwa na mazingira yanayomzunguka.

Ni lazima kuchuja kile kinachoingia akilini kupitia milango ya fahamu. Chujio lako liruhusu mawazo chanya tu! Mawazo chanya (furaha, upendo, ushirikiano n.k) ni mbolea/mtaji katika jihada za binadamu za kujiletea maendeleo.