Monday, February 27, 2012

KUTUNZA MGONJWA

Ni ukweli usiopingika ya kwamba, mgonjwa huwa na nafasi kubwa ya kupona au kupata nafuu haraka iwapo apata ushiriano wa kutosha kutoka kwa jamii inayomzunguka.

Pindi mtu anapofanyiwa uchunguzi wa kitabibu na kugundulika kwamba anatatizo, taratibu za matibabu hufuata. Ikiwa mgonjwa atakosa ushirikiano kutoka kwa jamaa, rafiki, ndugu n.k zake hukumbwa na hofu, woga, mtizamo hasi n.k. Hivyo hupungua kinga ya mwili na hatimaye kupunguza uwezekano wa kupona kwa haraka.

Ikiwa mtu atathibitika ni mgonjwa, jamii inayomzunguka (muuguzaji) inapaswa kufanya yafuatayo ili kufanikisha uponyaji:

1. Kumsikiliza mgonjwa.

Si wagonjwa wote hupenda kuongea, ikiwa yupo, anapaswa kusikilizwa kwa makini na upendo. Ikiwa mgonjwa hapendi kuongea, yapaswa ajengewe mazingira ya upole na utulivu wa akili ili aongee kwa uwazi.

2. Kuongea juu ya ugonjwa.

Wakati muafaka ukifika, mazungumzo juu ya ugonjwa yanapaswa kufanyika. Mazungungumzo yanaweza kuhusu ukubwa wa ugonjwa katika jamii husika, dalili na matibabu. Mgonjwa anahitaji taarifa sahihi juu ya ugonjwa ili kujiandaa kiakili juu ya hatua zinazofuata. Pindi mgonjwa anapoomba maoni kutoka kwa mlezi, muuguzaji atumie busara ili kutomkwaza mgonjwa.

3. Kutodharau.

Ni kawaida kwa wagonjwa kulalamika, hata wengine kumlaumu daktari au Mungu. Katika hali hii, mgonjwa asijibu au kutoa ishara za dharau au kebehi. Muuguzaji ajitahidi kujua sababu za majibu au hisia za mgonjwa, huku akimfariji.

4. Kumsaidia mgonjwa kazi.

Iwapo mgonjwa anapenda kusoma, kuandika, kuangalia TV, n.k asaidiwe ili atimize azma yake haraka iwezekanavyo. Yote kwa yote, mgonjwa anapaswa kusaidiwa majukumu ya siku kwa siku kama vile kufua nguo, kunyoosha nguo n.k ili kufanikisha usafi na kumwondolea mawazo.

5. Kuwezesha mawasilaino.

Muuguzaji anapaswa kumuunganisha mgonjwa na rafiki au ndugu zake. Ili kufanikisha mawasiliano, muuguzaji anapaswa kutoa taarifa juu ya hali ya mgonjwa kwa watu wa karibu. Kutoa taarifa kunarahisisha mawasiliano, pia huwezesha upatikanaji wa misaada kwa haraka.

6. Kusimamia utekelezwaji wa magizo.

Muuguzaji anapaswa kupokea na kusimamia kwa makini maagizo kutoka kwa nesi au daktari. Muuguzaji anapaswa kusimamia maagizo juu ya utumiaji wa dawa, ufanyaji wa mazoezi (kutembea), huduma ya kwanza n.k. Ili kurahisisha utekelezwaji wa maagizo, muuguzaji anapaswa kutunza maagizo yote anayoambiwa na daktari au nesi. Ikibidi kuwe na mawasiliano (simu) baina ya muuguzaji na Muuguzi.

Pia ni vizuri kumuomba Mungu kwa pamoja (mgonjwa na muuguzaji) kwani tafiti zimethibitisha kwamba wagonjwa hupata faraja na kupata nafuu/ kupona haraka pale sala zinapofanyika, sala za kuwaombea wapone haraka.
Neno muuguzaji linawakilisha mtu au watu wanaomhudumia mgonjwa siku kwa siku (iwe nyumbani au hosptali), na wala si Nesi.

Monday, February 20, 2012

JINSI YA KUEPUKA MADHARA YA TABIA HATARISHI

Kuna watu wengi waliyomo hatarini kutokana na mienendo yao mibaya. Watu wengi hususani vijana wamo hatarini kutokana na kunywa pombe kupita kiasi, kuvuta sigara, kufanya ngono kiholele, kutumia madawa ya kulevya n.k

Watu hawa wanafahamu wanayoyafanya ni hatari kwao na kwa jamii yao. Ni hatari kwao kwa kuwa huhatarisha afya zao, huvuruga uhusiano wao na jamii, hupelekeea kifo (mfano Whitney Houston) n.k. Mienendo mibaya ni mzigo kwa jamii kwa kuwa; jamii inabeba jukumu la kulea wahanga, hupunguza nguvu kazi, hupelekea uvunjifu wa amani n.k

Baadhi ya waathirika wa mienendo hasi hujaribu kujinasua, wachache kati yao hufanikiwa, ila wengi kushindwa kwa kuwa au wao au jamii yao imeshindwa kutoa msaada fasaha. Ikiwa mtu anataka kuondokana na tabia chafu, anapaswa kufanya yafuatayo:

1. Kudhamiria kuacha kama lengo kuu.

Pamoja na kuwa na rundo la malengo ili kufikia maisha bora, mwathirika anapaswa kuamua kuacha tabia chafu kama lengo namba moja. Mtu anapaswa kupanga kwa maandishi siku na saa ya mwisho kufanya jambo hatarishi. Ili kutorudia tena, mtu apange atakachofanya ili kufuta mawazo mabaya.

Inafaa kuacha kidogokidogo (hatua kwa hatua), kusitisha utumiaji wa madawa ya kulevya ghafla kunaweza kusababisha kifo. Mtu anaweza kusoma machapisho juu ya madhara, kushiriki michezo, kujiunga katika vikundi vya watu wema, kuwa karibu na watu sahihi, kuomba ushauri kutoka kwa viongozi wa dini n.k. Malengo yatizame waliofanikiwa kuliko walioshindwa.

2. Kuwazia mafanikio.

Mtu anapaswa kujenga picha ya maisha 'safi'. Kuwaza jinsi atakavyopata ujasiri, jinsi atakavyowekeza nguvu na rasilimali anazotumia kulipia huduma hatarishi. Jinsi mtu husika atakavyokubalika na kuaminika katika jamii, atakavyofaidi utajiri wa jamii yake n.k.

3. Kutafuta njia rahisi na sahihi.

Inafaa kutafuta mbadala wa maisha na ambao ni salama. Hii ikihusisha jinsi ya kuishi na kupata msaada kutoka kwa; ndugu, jamaa, marafiki n.k ambao hawana imani na mwathirika.

Mara nyingi inabidi mtu abadili marafiki, maeneo aliyozoea kukaa (vijiwe), kukataa kusikiliza baadhi ya miziki. Mtu kamwe! asibadili tabia moja dhidi ya nyingine, mfano kunywa pombe kupindukia isiwe mbadala wa kufanya ngono.

4. Kukataa mitizamo hasi

Ili kufanikiwa, mtu anapaswa kukataa mitizamo hasi na misemo kama "kuacha haiwezekani, huu ni ulevi wa kawida, kila mtu ana ulevi wake" n.k. Mitizamo hiyo hasi hufutika kwa kujiambia mara kwa mara "naanza leo na nitapata mafanikio haraka, nitajitahidi kutunza afya yangu, mbona nanii..ameweza, hakuna lisilowezekana" n.k

5. Kujizawadia

Waswahili wanasema "raha jipe mwenyewe babu/ bibi....". Hivyo, ikiwa malengo yamefikiwa kwa kiasi fulani, mtu anapaswa kujipongeza. Zawadi inaweza kugharamiwa kwa fedha zilizokuwa zikitumiwa kulipia huduma angamizi. Mtu anaweza kujipongeza kwa kununua thamani, kutalii, kufanya sherehe na rafiki zake, kusaidia wasiojiweza, kusaidia waathirika wenzake n.k. Kujizawadia huleta uhalisia wa mfanikio ya siku za mbele.

6. Kutafuta msaada,

Watu wenye uwezo mdogo wa kufikiri husema "tabia ni kama ngozi (haibadiiki), kafiri haachi asili" n.k. Watu wanaotaka na kusababisha mabadiliko husema; tabia hubadilika kulingana na mazingira, utayari wa kuacha na msaada kutoka kwa jamii.

Ili kupata mafanikio ya haraka, mtu anapaswa kuomba ushauri kutoka kwa waliofanikiwa kuacha, wataalamu wa ushauri nasaha, viongozi wa dini, kujiunga na vikundi vya wanaharakati, kuonyesha kwa vitendo dhamira ya kutaka kuacha pamoja na kumshirikisha Mungu.

7. Kuweka rekodi ya mafanikio.

Mtu anapaswa kuweka rekodi kutokana na mafanikio aliyoyapata kutokana na malengo. Kabla ya kulala na kuamka, mtu asome mafanikio ya siku za nyuma. Huku akiweka mikakati juu ya kukabiliana na changamoto za siku kwa siku. Mikakati hiyo iwe ya kawaida na inayotekelezeka kulingana na mazingiza na uwezo wa mtu husika.

8. Kumiliki mihemko.

Watu hupata changamoto kuu siku chache baada ya kuacha iliyokuwa burudani yao. Wengi wao hupata homa, kuarisha, kutapika, kusikia kizunguzungu, kukosa usingizi n.k kwa kuwa wameacha kutumia madawa ya kulevya au pombe kali au sigara.

Bahati nzuri ni kwamba mtu hawezi kufa hususani kama atakula mlo kamili (hususani mboga mboga na matunda) pamoja na maji ya kutosha. Pia mawasiliano ya mara kwa mara kati ya mwathirika na mlezi wake ni muhimu sana. Inapendekezwa mlezi awe ni mtumiaji aliyefanikiwa kuacha.

MCHANGO WA JAMII NI MUHIMU SANA KATIKA KUOKOA WATU WALIOMO HATARINI, WENGI WAO HUTAKA KUACHA LAKINI JAMII HAITAKI. JAMII HAITAKI KWA KUENDELEA KUWABAGUA NA KUTOWAPA USHIRIKIANO.

Monday, February 13, 2012

HOFU KATIKA MAISHA

Hofu au ujasiri ni sehemu ya maisha ya mtu yeyote yule! Kiwango cha hofu au ujasiri hutofautiana kulingana na hisia za mtu. Hisia alizo nazo mtu hutegemea mawazo yake pamoja na mfumo wa kibailojia (homoni).

Hisia hasi za mtu hujengeka kwenye misingi ya woga, ujinga, kutojiamini, n.k. Kwa upande mwingine, hisia chanya hujengeka kwenye misingi ya ufahamu, imani, kujiamini, ujasiri, n.k.

Hofu aliyo nayo mtu yeyote huwa ni mchanganyiko au sehemu mawazo juu ya vitu sita ambavyo ni; kufilisika, kulaumiwa, ugonjwa, kuachwa na mpenzi, uzee na kupoteza maisha.
Mawazo juu vitu hivyo pamoja na suluhu zake ni kama ifuatavyo:

1. Hofu ya kufilisika.

Mtu anaweza kupata hofu ya kupoteza mali alizochuma (hata kupoteza kazi). Hofu hii huwakumba sana watu 'wanaoabudu' mali au hela. Watu hawa hutumia muda wao mwingi kutafuta mali ili kujiimarisha. Watu hawa hutegemea wingi wa mali zao ili kupata amani maishani.

Watu hupata hofu ya kufilisika mara baada ya kuona au kupewa mifano halisi ya watu waliokuwa na mali nyingi na sasa wamefilisika (wamefulia ile mbaya).

Hofu ya kupoteza mali inaweza kuepukwa kwa mtu kukataa kuwa mtumwa wa mali za dunia hii. Mtu anapaswa kuhakikisha anatumia mali na si mali zimtumie yeye. Kila mtu anapaswa kufahamu kwamba mali zake zinaweza kutoweka; kama itatokea awe tayari kuikubali hali hiyo ili aweze kuishinda. Pia ni vizuri kuwa na mahusiano mazuri na ndugu, jamaa na jamii inayomzunguka mtu

2. Hofu ya kulaumiwa.

Takribani watu wote hufanya au kuhakikisha utekelezaji mambo ili wapate sifa kutoka kwa jamii au kundi fulani la watu. Hivyo, hawajiandai kwa ajili ya kudharauliwa, kutusiwa n.k kutokana na maamuzi au yao au ya kundi. Kuogopa lawama kunawafanya watu waogope nafasi za uongozi, kutoa mawazo yao au kukosoa mambo yasiyo sahihi pale wanapotakiwa kufanya hivyo.

Kuogopa lawama kunaweza kuepukwa kwa kusikiliza na 'KUTATAA' yale mtu anayoambiwa juu ya ugumu wa jambo fulani. Mtu anapaswa kuamini mawazo aliyopewa na watu sahihi na anayotekeleza kulingana na hali yatampa tuzo.

Pia mtu afahamu watu wanaomkosoa wana; lengo gani, elimu, au uzoefu gani juu ya jambo husika, kama wanalenga kujenga au kubomoa n.k. Ikiwa watu wangeogopa lawana wasingefanya mambo ya maana kwao au kwa jamii zao. Lawama ni miongoni mwa mavuno, na lawama hazikwepeki.

3. Hofu ya ugonjwa.

Kuna nyakati fulani watu hupata hofu juu ya afya zao. Watu hupata hofu ya homa fulani kwa sababu ya kutokuwa na elimu juu ya ugonjwa, kuona watu walioathirika na ugonjwa fulani, kutofuata kanuni za afya wakati wa kufanya jambo fulani(mfano kushiriki ngono isiyo salama) n.k. Mtu anaweza kupatwa na mafua akahisi ana Kifua Kikuu, UKIMWI.....

Hofu ya homa au ugonjwa fulani inaweza kuondolewa kwa kutafuta habari sahihi za ugonjwa husika, kupata ushauri, kupima, kufuata kanuni bora za maisha kama; mapenzi salama, kunywa maji safi na salama, kufanya mazoezi ya viungo, kula mlo kamili n.k

4. Hofu ya kupoteza penzi.

Mtu anaweza kupata hofu juu ya mwenendo wa kimapenzi wa mpenzi wake baada ya kuambiwa maasi ya kimapenzi yanaoyafanywa na marafiki wa mpenzi wake, kusimuliwa mikasa ya kimapenzi, kuhisi kama anasalitiwa na mpenzi wake n.k. Hofu ya kupoteza penzi kumfanya mtu aamini mapenzi yananunuliwa au kuchukia jinsia nyingine.

Ili kuepuka hofu ya kupigwa chini, mtu anapaswa kuwa karibu na mpenzi wake ili apate kujua ukweli wa mambo, kukumbuka mambo mazuri aliyoyafanya na mpenzi wake, kuchuja anachoambiwa na marafiki zake kuhusu mpenzi wake n.k. Mtu anapaswa kuamini penzi halipotei; kwani penzi ni muendelezo usioisha wa hisia baina ya mtoaji na mpokeaji. Kuaminiana ni suluhu kuu ya hofu ya kupoteza penzi.

5. Hofu ya uzee.

Watoto wadogo hupenda kukua na kuitwa watu wazima. Watu wazima hukataa utu uzima na ambao ni lazima kwa viumbe hai wote. Watu huogopa uzee kwa kuwa wanaihisi watapoteza mvuto, watapitwa na 'wakati', kuzeeka kutawafanya kutofurahia maisha, kupatwa magonjwa ya uzeeni n.k

Kutokana na hofu ya kuzeeka, baadhi ya watu hupenda kuvaa, kuongea, kutumia vipodozi vya ngozi na nywele ili waonekane ni vijana. Baadhi ya watu hupenda kujihusisha na makundi ya vijana; na kuwaacha watu wa umri wao.

Ili kuepuka hofu ya kuzeeka, mtu anapswa kujua ya kwamba kuwa na umri mkubwa katika jamii ni hazina, ni dalili ya kukua, watu wazima huwa na busara na hekima kwa ajili ya kulea jamii (vijana) kwa kuwa mienendo yao bora na ya kuigwa. Uzee ni tunu kutoka kwa Mungu.

6. Hofu ya kupoteza maisha.

Baadhi ya watu hupata hofu ya kupoteza maisha baada ya: kuona mwili au jeneza la marehemu, kuona kaburi, kuugua kwa muda mrefu, kuwaza juu ya kufa. Watu wengine hupata hofu ya kufa baada ya kukata tamaa ya maisha, kukosa kazi, kukosa watu wa kuwalea, kutengwa na jamii, rafiki zao (hasa wa utotoni) kufariki, kusikia magonjwa ya ajabu na yasiyo na tiba yakiua watu wengi n.k

Hofu ya kupoteza maisha huwafanya baadhi ya watu kutotia bidii katika shughuli za uzalishaji mali, kuuza mali walizochuma au kufuja mali zao hatimaye wao au jamii inayowategemea huingia kwenye dimbwi la umasikini wa kupindukia.

Ili kuepuka hofu ya kufa, mtu anapswa kujua kufa ni sifa ya viumbe hai vyote; hata Yesu, Musa na manabii maarufu walikufa. Pia mtu anapokufa hubaki akitukuzwa kwa yale mema aliyosema na kutenda, kwa msimamo wake katika kuleta mabadiliko kwa familia au jamii yake. Mali alizochuma mtu wakati wa uhai wake zitawakilisha uwepo wake hapa duniani.
HOFU ZOTE NI HISIA ZA AKILI, IKIWA MTU ATAZIENDEKEZA ATAANGAMIA!!!...

Monday, February 6, 2012

HUJUMA AFANYAZO MTU DHIDI YA NAFSI YAKE

Maria Robinson: "Hakuna mtu yeyote anayeweza kurudisha muda nyuma au kufuta historia ili aanze upya, ila mtu yeyote anaweza kuanza leo na kuandika ukurasa mpya wa mafanikio". Mtu yeyote anaweza kuanza mchakato wa kuboresha maisha yake wakati wowote ule, kama tu AKIDHAMIRIA kufanya hivyo.
Kwa bahati mbaya, watu huanza harakati za kupambana na maisha duni huku "wakikumbatia hujuma" dhidi ya nafsi zao. Hujuma hizo ni kama zifuztazo:

1. Kujihusisha na mtu au watu wasiosahihi.

Maisha ni mafupi sana, hususani ikiwa mtu anatumiwa kumnufaisha mwingine. Ikiwa mtu anahitaji msaada, atajenga mazingira ya kupata msaada. Watu wasiosahihi (wanyonyaji) hujenga mazingira ya kuwatumia wanyonge (maskini) ili kujinufaisha.

Watu hawa hujenga au kuimarisha uhusiani wakiamini tu! watapata msaada ili watimize malengo yao, huwatumia wanyonge kama ngazi, (mfano kuwapa msahara duni, kuwatumikisha zaidi ya uwezo n.k) bila kujali mustakabali wa afya n.k wa wanaowatumia. Mabosi hawa hawapo tayari kutoa msaada wa hali au mali ili kuwakwamua wafanyakazi wao.

Kwa hahati mabaya au kwa kujua au kwa kutojijua vibarua "huwaabudu mabosi hawa wanyonyaji na ambao huwatelekeza pindi wanapozeeka au kupata matatizo makubwa ya kiafya. Hatimaye vibarua huishia kuishi kama ombaomba wa kutupwa.

2. Kukimbia changamoto.

Ni vigumu sana mtu kukwepa changamoto zote zinazomkabili. Hivyo mtu anapaswa kusimama imara dhidi ya dhoruba za kimaisha. Watu hufanikiwa kwa kupitia changamoto moto moto. Kufanikiwa huwa ni matunda ya kukubali, kujifunza na kutatua changamoto zinazowakabili wakati wa kipindi chake chote cha maisha yao.

Watu hufanya hujuma dhidi ya nafsi au jamii kwa kukimbia changamoto bila ya kujua ya kwamba, changamoto zipo kwa ajili ya watu na watu ndio wao au bila ya kujiuliza, je watakimbia changamoto ngapi ili wafanikiwe?

3. Kujidanganya.

Mtu anaweza kumdanganya yeyote kaika dunia hii, lakini hawezi kujidanganya yeye mwenyewe. Maisha ya mtu huimarika pale anagundua na kuchangamkia fursa. Moja ya kitu kigumu ni kuukubali ukweli, ukweli ambao ni mlima ambao mtu anapaswa kuupanda ili afikie 'kilele' cha mafanikio.

Watu husaidiwa na mazingira au wale wanaowazunguka ili kujidanganya. Baadhi ya watu hujidanganya wana maisha mazuri ili hali hawajui au hawajapanga kesho au kesho kutwa yake itakuwaje, hawajafanya jitihada zozote kujikwamua.

4. Kujirudisha nyuma.

Baadhi ya watu (watu walio wengi) hawapo tayari kusimama mstari wa mbele huku wakipigania haki zao, hawapo tayari kusimama imara wakati wa kuwasilisha na kufafanua madai yao; huwaachia wawakilishi ambao si wahanga kupeleka hoja na kuwatetea (hata kwa mambo wanayoweza kuyafafanua wao wenyewe), wao hukaa na kusubiri taarifa za msuguano kutoka wa wanyonyaji kupitia wawakilishi.

Kwa bahati mbaya zaidi, baadhi ya watu huridhia haki zao zinyakuliwe wakiamini Mungu ndiye mtoaji. Kila mpiganaji anapaswa kuwa na roho ya kibinadamu, lakini asijishushie hadhi kwa kujiweka 'mkiani' au kijidharau.

5. Kufuata mkumbo.

Moja ya changamoto zinazomkabili mtu popote pale anapoishi ni kutaka kuishi maisha yake, maisha yasiyo na ushawishi kutoka kwa kundi fulani la watu katika jamii.
Kutokana na changamoto hiyo, watu hujikuta wakijidhulumu kwa kuiga maisha (kufuata mkumbo) ya watu waliofanikiwa wakiamini nao watafanikiwa au ili wapate kukubalika.

Watu wa ukweli ni wale wanaoweka vigezo vyao, kwa kuzingatia uwezo wao; vigezo wanavyoamini vitawatoa kimaisha. Vigezo au vipaumbele vitakavyowafanya wawe maarufu kwa mali, maelewano, mahusiano na jamii yao; si kwa mawazi, kuhudhuria klabu au vipodozi n.k

6. Kuogopa makosa.

Kufanya kitu bila ya kufanikiwa (kwa makosa) hata mara mia ni bora kuliko kutofanya chochote. Kila aliyefanikiwa ameanguka mara nyingi, na kila anguko limenfanya mtu aimarike zaidi. Baada ya kufanya jitihada za bila matunda yanayoridhisha, mtu hufanikiwa.

Kwa mfano, mwanasayansi aliyegundua balbu ya umeme alifanya majaribio mara 3000 na hatimaye akafanikiwa kutengeneza balbu inayowaka. Hata alipotakiwa na wanahabari kueleza palipokuwa panamshinda hivyo kufanya majaribio mengi aliwaambia "sijui tatizo lilikuwa ni nini".

7. Kununua furaha.

Watu hujidanganya ya kwamba wakimiliki kitu/ vitu fulani vya thamani au kujihusisha na mtu/ watu fulani watakuwa na furaha maishani. Hivyo, hutumia muda nwingi au rasilimali zao kugharamia furaha. Baadhi ya watu hudiriki kununua baadhi ya bidhaa za gharama, kugharamia mitoko na watu maarufu au kutafuta mahusiano ya kimapenzi na watu maarufu ili furaha yao itimie. Mwishowe hupata mgogoro wa nafsi na si furaha.

Ukweli ni kwamba, vitu vya kawaida ndivyo vinavyoleta furaha ya kweli na ya kudumu; vitu au mambo anayafanya mtu kwa hiari ya moyo na akili yake; vitu ambavyo vipo ndani ya uwezo wa mtu.

8. Kutoishughulisha akili.

Mtu asiyefikiri kwa ufasaha ndiye anayetekwa au kutumiwa na shetani kutekeleza uovu. Kila mtu anapaswa kuchambua kwa kina hali aliyonayo na kuchukua hatua sahihi.

Mtu anapaswa kuitumikisha akili ili kupata ya mambo aliyowahi kuambiwa hayawezekani. Kusonga mbele ni kukubali kukabili hatari. Pia mtu asiwaze (asiwaze bila mapumziko) kiasi cha kupata msongo mawazo.

9. Kuamini ukamilifu.

Wapiganaji hawaamini wamefanikiwa kwa 100% hata wapate fursa nzuri kiasi gani! Baadhi ya watu hubweteka kwa mafanikio kidogo, wakiamini wamefikia kilele, wengine huridhia kuacha kazi zao za ziada. Mabilionea hulazimishwa na mafanikio kufanya kazi zaidi; huku wakiamini mafanikio waliopata ndio mwanzo tu, na wanapaswa kutafuta fursa bora zaidi.
AMUA KUACHA HUJUMA LEO!