Monday, August 20, 2012

VIKWAZO DHIDI YA USINGIZI MURUA NA SULUHU ZAKE

Usingizi ni moja kati ya vitu muhmu kwa afya ya binadamu. Kukosa usingizi ipasavyo (masaa 6-8) hupelekea matatizo kama uchovu siku inayofuata, kusinzia siku inayofuata, kupungua uzito, kupungua kinga ya mwili n.k. Kuna imani potofu ya kwamba watoto ndio wanaopaswa tuu kulala muda fasaha.

Kwa kuwa watu wengi hawapo makini katika kuangalia mienendo ya maisha yao, hawawezi kujua sababu zinazopelekea matatizo hayo, hivyo kukosa sululuhu ya kudumu. Zifuatazo ni sababu zinazopekea ukosefu wa usingizi, baada ya kuzijua itakuwa rahisi kwa mtu kukabiliana na changamoto.

Kula chakula kingi muda mchache kabla ya kulala.

Kula chakula kingi, hususani nafaka, muda mfupi kabla ya kulala hufanya mwili utumie nishati nyingi katika kumeng'enya chakula, hivyo kuvuruga utaratibu wa nishati wa mwili. Pia kunywa maji kabla ya kulala humfanya kuamka usiku ili kujisaidia, hivyo kubadili utaratibu wa usingizi.
Mtu anapaswa kula chakula chepesi na maji kidogo angalau nusu saa kabla ya kulala.

Kulala mazingira duni.

Kulala katika mazingira yanayokinzana na utu wa mtu huvuruga utaratibu wa mwili. Mazingira kama; chumba chenye mwanga mkali, chumba chenye joto au baridi kali, kulala kwenye kelele, kulala kwenye godoro laini au gumu sana, chumba kisicho na hewa safi ya kutosha n.k humfanya mtu kukosa usingizi.

Kubadili mfumo wa maisha.

Kubadili mfumo wa maisha na ambao ulikuwa umezoelewa na mwili hutatiza usingizi. Kwa mfano; kumpoteza ndugu au rafiki wa karibu, kuanza kazi mpya, kufanya kazi ngumu, kuingia kwenye ndoa, kuwa na msongo mawazo n.k huwafanya watu wengi kukosa usingizi.
Hali hii huchukua siku chache, ikiwa kama ukosefu wa usingizi itachukua muda mrefu, mtu anapaswa kufanya tahtmini ya kina.

Mazingira duni ya kijamii.

Mazingira duni ya kijamii kama; kulala zaidi ya mtu mmoja kwenye kitanda kimoja, kulala na mtu msumbufu hususani mtoto mdogo, kulala chumba kimoja na mtu anayekoroma, kulala na mtu anayesumbua usiku, kulala chumba chenye wadudu kama chawa, kunguni, viroboto n.k.
Mazingira haya yanasababishwa na umasikini wa kipato.

Matumizi ya madawa.

Kuna aina nyingi sana ya madawa ya hosptalini ambayo, pamoja na kutibu au kupunguza maumivu, hupelekea kukosekana kwa usingizi. Madawa hayo ni kama madawa ya kupunguza maumivu, kupunguza mawazo, madawa ya usingizi n.k.
Mtu anapaswa kusoma maelekezo au kupata ushauri wa daktari kabla ya kutumia dawa yoyote ile ili apate kujua madhara yake na jinsi ya kuyakabili.

Matumizi ya vinywaji baridi na sigara muda mchache kabla ya kulala.

Vinywaji baridi vina kokaini, chai au kahawa ambayo huongeza msukumo wa damu. Matumizi ya vinywaji hivyo kabla ya kulala kukatiza usingizi. Kwa upande wa sigara, ikilinganishwa na watu wasiovuta sigara, watu wanaovuta sigara hukawia kupata usingizi, hivyo, kupata masaa machache ya kulala.
Kuna watu wamezoea kunywa pombe ndipo wapate usingizi, watu hawa ni watumwa wa pombe na wengi wao hutumia pombe kali, baada ya muda, pombe haitoweza kumsabishia usingizi kabiasa au akiwa hana hela ya kununua pombe mtu huyo hatoweza kulala.

Kwa kiasi kikubwa, sababu za ukosefu wa usingizi zipo chini ya uwezo wa binadamu, hivyo, mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla inapaswa kutengeneza mazingira yanayopekekea usingizi murua, mafanikio ya mtu katika kazi za kujiletea maendeleo, hutegemea, pamoja na mambo mengine, kiasi cha mapumziko anayopata kila siku kupitia usingizi.

Monday, August 13, 2012

MUUNDO WA MPANGO WA MAENDELEO

Watu wengi hushindwa kufikia malengo waliyojiwekea kwa kuwa, moja ya sabau ni, kushindwa kupanga. Kushindwa kupanga hupelekea kushindwa kutekeleza hivyo malengo kutikiwa. Zifuatazo ni hatua muhimu za kumsadia mtu pindi apangapo mradi wa maendeleo.

1. Kununua kitabu cha mipango. Mtu anapaswa kununua kitabu kidogo kwa ajili ya kuratibu na kutunza kumbukumbu za kila siku za mtu binafsi. Vitabu hizi vipo takribani kila duka la vifaa vya shule na ofisini, hujulikana kama "diary" kwa lugha ya Kiingereza.

2. Kuandika mtizamo, lengo au matarajio ya mradi husika. Mtu anapaswa kuandika mradi wake kwenye ukurasa wa kwanza wa kitabu cha mipango. Lengo husika linapaswa kuandikwa kwa herufi kubwa na kwa lugha fasaha. Kwa mfano, LAZIMA NIANZISHE MRADI WA UFUGAJI WA KUKU WA KIENYEJI IFIKAPO MWEZI JANUARI MWAKANI . Mtu anapaswa kuhakikisha anaandika lengo moja tu! Ili iwe rahisi kutekeleza.

3. Kuandika kwa kifupi shughuli muhimu zitakazofanyika na muda mahususi wa kuzifanya ili kufikia lengo kuu. Shughuli hizo hujumuisha malengo madogo madogo. Kwa mfano:

Ni lazima nianzishe mradi wa ufugaji wa kuku wa kienyeji kabla ya mwezi Januari mwakani. Ili kufanya hivyo ninapaswa kufanya yafuatayo; (i) kuomba ushauri kutoka kwa mfugaji maarufu wa kuku wa kienyeji juu ya gharama muhimu wiki ya tatu ya mwezi Agosti (ii) kukamilisha gharama muhimu za kuanza mradi kabla ya wiki ya nne ya mwezi Agosti, kama ikibidi (iii) kuomba ushauri kutoka kwa Afisa Mifugo juu ya aina bora ya kuku, magonjwa n.k wiki ya kwanza ya mwezi Septemba (iv) kufanya utafiti juu ya upatikanaji wa soko la kkienyeji ndani ya wiki ya pili na tatu ya mwezi Septemba (v) kuanza kujenga banda wiki ya tatu ya mwezi Septemba na kukamilisha kabla ya mwisho wa mwezi Oktoba (vi) kununua chakula na dawa muhimu wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi Novemba (vii) kununua kuku wa kienyeji; mitetea nane na jogoo mmoja wiki ya kwanza ya mwezi Desemba. Hivyo kuanza ufugaji rasmi kabla ya mwezi Januari.

Mpangilo wa shughuli na muda hutegemea mazigira, uelewa wa mtu, rasilimali akizo nazo n.k. Kwa mfano, kupata mtaji kwa mtu mmoja ikawa changamoto ili hali, kwa mtu mwinine kupata ushauri ikawa changamoto kuu.Mtu apange shughuli rahisi kisha shughuli ngumu baadaye kadiri ya uwezo wake. Ni bora kumshirikisha mtu wa karibu ambaye nimzoefu wakati wa kupanga ili kuepuka kupanga shughuli isiyotekelezeka ndani ya muda fulani.

4. Kurudia kusoma, kufanya marekebosho na kukariri mwongozo ulioandaliwa. Muongozo uwekwe maeneo ambayo ni rahisi kuuona na kuusoma kama kwenye pochi au kwenye mkoba. Hii itaongeza hamasa ya kusoma na kutaka utekelezaji.

5. Kuanza utkelezaji kwa kuandaa ratiba ya hughuli iliyopangwa kufanyika ndani ya muda husika. Katika hatua hii mtu anapaswa kuwa makini sana ili asiruke shughuli aliyoipanga. Ikiwa kama shughuli husika haikuisha ndani ya muda uliopangwa, basi ipelekwe mbele. Kuruka hatua kutasababisha kuvuruga mpango mzima.

6. Kufanya uchambuzi wa hatua kwa hatua. Mtu anapaswa kuangalia utekelezwaji hatua iliyopita ili kufanya marekebisho kwa hatua zitakazofuata kabla mambo hayajawa magumu. Mwenye mradi anapaswa kuwaongoza kwa makini wasaidizi wake wa kila siku.

Monday, August 6, 2012

VIASHIRIA VYA BAHATI

Watu wengi hufikiri ya kwamba bahati (nzuri au mbaya) hujijia tu, haibashiriki na ni vigumu kuzuia. Hiyo ni kwa kuwa hawajui maana halisi ya bahati. Ikiwa kama mtu hajui maana halisi ya bahati ni vigumu kuitawala. Waswahili wanasema "mtembea bure si sawa na mkaa bure" pia "bahati ya mbwa ipo kwenye miguu yake".

Bahati ni kujitambua dhidi ya uhalisia. Bahati ni kuwa na hisia chanya juu ya tukio au jambo fulani. Mtu mwenye hisia chanya huona kila kitu kinamtumikia (kila kitu kinamsadia kufanikiwa), kwa upande mwingine, mtu mwenye hisia hasi huona kila kitu kinampiga vita; kila kitu huonekana ni kikwazo.

Kiasi cha imani (nguvu itokayo ndani) huamua kiwango cha hisia na bahati ya mtu. Mtu anapofanya jambo lolote pasipo imani, kufanya jambo kwa mashaka makubwa, huwa na uwezekano mkubwa kufanya makosa ya kizembe hivyo kujiweka katika nafasi kubwa ya kungeza vikwazo au kukosa kabisa kile alichotaka. Pindi mtu anapojiamini kwa kiasi kikubwa ndipo uwezekano wa bahati (kufanikiwa) unapoongezeka.

Kwa kiasi fulani, bahati hutegemea maarifa. Mtu mwenye maarifa hufanya kazi kwa uhuru. Ni vigumu kutenganisha bahati na maarifa; kwani ili kufanya kitu kwa usahihi uwezo wa mtu husika kufuata sheria na kanuni ipasavyo unahitajika.

Kwa kuwa bahati hutegemea imani, mtu anapaswa kuwa makini na kiwango cha imani yake wakati anapofanya jambo lolote lile. Ikiwa kama kiwango cha imani ni kidogo, yafaa kusitisha kufanya jambo hilo, au kufanya hatua kwa hatua na kwa umakini mkubwa kama haiwezekani kusitisha shughuli husika.

Watu wanaolazimisha kufanya jambo bila ya imani nalo hujikuta wakifanya makosa bila ya kujitambua, kusahau hatua za kufuata, kushindwa kujitetea pindi wanapotakiwa kijitetea, hivyo kubaki wakijilaumu kwa kujisemea "nina bahati mbaya".

Kukosa umakini kimawazo huwafanya watu kudharau mambo ya msingi; kujikuta wakifanya mambo wasiyotayatarajia kisha kutokufanikiwa. Ili kuongeza nafasi ya bahati ya kufanikiwa yapaswa kuwekeza kimawazo, kushirikisha maarifa kwenye kazi ifanyikayo kwa wakati husika. Kuwekeza kimawazo husaidia kutumia rasilimali kwa ufanisi zaidi.

Takribani watu wote (wanasayansi mashuhuri, wafanyabiashara wakubwa, wasomi n.k) waliofanikiwa, walifanikiwa kwa kuwa kiwango chao cha imani kilikuwa juu. Kufanya kazi bila ya i tiketi ya kushindwa. Mtu anayetaka bahati nzuri huchagua mtizamo chanya, mtizamo chanya huongeza nishati na kusadia jitihada za kufanikiwa.

Kila mtu anayo nafasi ya kufanikiwa, watu wengi hawajui maana na jinsi ya kulinda nafasi wanazopata katika maisha. Bahati nzuri ipo, na kila mtu anao uwezo wa kuitawala. Kwa kulitambua hilo, hakuna haja ya kuogopa kufanya jambo lolote kwa kuwa hakuna bahati mbaya.