Monday, October 3, 2011

HATUA SITA ZA KUWA JASIRI

Watu wengi wana uwezo wa kufanya mambo makubwa na yenye kuleta mafanikio, wanakosa mafanikio kwa kuwa hawana ujasiri wa kuwaza na kufanya maamuzi.
Njia zifuatazo zinasaidia kuimarisha uwazaji na kuwezesha kuchukua hatua zitakazowezesha kufikia malengo.

Hatua Ya 1: Chukua Hatamu Ya Maisha Yako
Kujali kile watu wanachosema juu yako ni kuwapa nafasi watu wayaongoze maisha yako badala yako.
Kujali watu wanachowaza ni utumwa unaowakabili watu wengi. Wengi tumelelewa (kwa nia njema) tukijali mawazo ya wengine zaidi, kitu kinachopelekea kuwa katika maisha, kazi n.k yasiyo na furaha wala mafankio.

kutaka kuwaridhisha wengine wakati wote ni tatizo linaloanza utotoni ili kukubalika. Hali hii huimarika ukubwani kiasi kwamba mtu anakosa kujiamini na kutanguliza mbele kile wanachowaza wenzake na si matakwa au mahitaj yake. Hali hii hupelekea umasikinii wa mawazo na hatimaye wa kipato.

Kabla ya kufanya chochote , jiulize, je unafanya kwa makusudio yako au ili kuaridhisha marafiki, ndugu n.k?
Kufuata mawazo ya wengine kunamfanya mtu kuwa; mtumwa, kunaua ubunifu na kumaliza nguvu za kutekeleza malengo binafsi, kunazuia mtu kwenda anapotaka, kufurahia anachotaka na hatimaye kukosa mafanikio anayotaka.

Hatua ya 2: Jitahidi Kuwa Tofauti
Karibu kila mtu anajitahidi kuwa sawa (sawa na marafiki, tabia, tamaduni n,.k) ili apate kukubalika katika jamii husika.
Inapasa mtu kuchambua mienendo yote kwa kina kujua kama "usawa" anaoutaka utaleta mafanikio au la!
Kama ni wa kufuata mkumbo, hatua za haraka zichukuliwe ili kuepusha utumwa au utekwaji nyara na mambo yatakayorudisha nyuma jitihada za kimaendeleo.

Hatua ya 3: Tazama Mbele
Ikiwa mtu atabaki kulaumu makosa aliyofanya awali, ajue anaua kujiamini na kushindwa kusonga mbele. Makosa ni mazuri (mtaji) kama yatachambuliwa ipasavyo (yakichambuliwa chanya au kama somo)

Kama mtu anataka kuwa jasiri, asichukue makosa kama makosa bali, kama masoma muhimu katika maisha. Hii itasaidia kujenga mustakabali wenye mafanikio.
Ili kufanikiwa haipaswi kukatishwa tamaa na idadi ya makosa. Kukosa ni muhimu ili kujua nini cha kufanya au kutofanya wakati fulani. kufanikiwa au kutofanikiwa ni suala la kimtazamo.

Hatua ya 4: Amini "Bado Sijachelewa"
Kuna watu wengi hawapendezwi na kazi wanazofanya kwa muda mrefu, lakini wanakosa ujasiri wa kuziacha kwa kuwa wanahisi wamechelewa kuanza au kujifunza fani/kazi nyingine.

Kama mtu analo lengo fulani, lakini anajikuta akijiambia "nimechelewa", njia pekee ya kuvua woga huo na kuvaa ujasiri ni kutouzingatia na kukabili kile anachokiogopa kwa nguvu zote.

Hatua ya 5: Kutojiwekea Ulinzi
Kuna wasomi wengi wamekosa mafanikio kwa kuwa kila wanachowaza kufanya wanawaza kwa tahadhari ya hali ya juu. Hali ambayo inawanyima uhuru.

Kuna watu wanaoweza kufanya biashara lakini hawana ujasiri wa kuthubutu, wanaogopa hasara kama kuwaka moto, kuibiwa n.k hivyo hutumia muda mwingi kufikiria juu ya kampuni za ulinzi, bima au tahadhari nyingine.

Ili kuepuka kujiwekea ulinzi uliopitiliza inapaswa kuthubutu. Kuthubutu yafutayo:
¤kuthubutu kuwa kuwa peke yako
¤kuthubutu kuwa na mtindo wako wa maisha na si kufuata mitindo ya kundi fulani bila sababu za msingi
¤kuthubutu kusoma na kufanya kazi kwa bidii ili kuimarisha fani husika
¤kuthubutu kuwa na mtazamo chanya na ujasiri wa kujaribu.

Hatua ya 6: Amini Utafanikiwa
Daima dumu! Kufanikiwa au kutafanikiwa kunategemea mtu anavyowaza na kuamini. Hivyo ili kuwa na ujasiri mtu anapaswa kuamini kwamba kuna kufanikiwa, huku akifanya mambo yanayopelekea mafanikio.

Ili kuvunja minyororo na utumwa wa mawazo "nitashindwa" yafaa:
¤kuchati chanya kimoyo-moyo
¤kujihusisha na watu wanaowaza kufankiwa au waliofanikiwa
¤kuwaza "nami" naelekea kufanikiwa
¤kuwaza "mimi" ni mshindi.

Mtu anapaswa kujishawishi yeye mwenyewe. Watu humshauri mtu juu ya kufanikiwa baada baada ya yeye binafsi kujishauri.

1 comment: